• HABARI MPYA

    Monday, June 04, 2018

    SIMBA SC YAIFUTIA AIBU TANZANIA, YATINGA NUSU FAINALI SPORTPESA SUPER CUP

    Na Mwandishi Wetu, NAKURU
    MABINGWA wa Tanzania Bara, Simba SC leo wamefanikiwa kuingia Nusu Fainali ya michuano ya SportPesa Super Cup baada ya ushindi wa penalti 3-2 dhidi ya Kariobangi Sharks kufuatia sare ya 0-0 ndani ya dakika 90 Uwanja wa Afraha mjini Nakuru.
    Shujaa wa Simba SC leo alikuwa ni kipa wake hodari, Aishi Salum Manula aliyeokoa penalti mbili za Kariobangi Sharks na sasa Wekundu hao wa Msimbazi watakutana na Kakamega Homeboys katika Nusu Fainali.
    Waliofunga penalti za Simba SC ni Haruna Niyonzima, Erasto Nyoni na Jonas Mkude, wakati Mohammed Hussein 'Tshabalala' na Paul Bukaba walikosa.
    Simba SC pia imeifutia aibu Tanzania baada ya jana Yanga SC na JKU ya Zanzibar kutolewa na  timu za Kenya katika hatua ya kwanza tu ya michuano hiyo.

    Wachezaji wa Simba SC, Moses Kitandu (kulai) na Shiza Kichuya (katikati) wakimpongeza mwenzao, kipa Aishi ManuIa aliyeokoa penalti  

    lianza Yanga SC kuchapwa 3-1 na Kakamega Homeboyz hapo hapo Uwanja wa Afraha mjini Nakuru, mshambuliaji wa zamani wa Azam FC, Allan Watende Wanga akifunga mabao mawili dakika za 26 na 30 na linguine la Kakamega Homeboyz likifungwa Wycliffe Opondo dakika ya 85, huku la timu ya Jangwani mjini Dar es Salaam likifungwa na Matheo Anthony dakika ya 38.
    JKU nayo ikafuatia baada ya kuchapwa 3-0 na mabingwa watetezi, Gor Mahia mabao ya George Odhiambo, Godfrey Walusimbi na Meddie Kagere na sasa wanapanda ndege moja na ndugu zao, Yanga SC kurejea Dar es Salaam kila timu ikipatiwa kifuta jasho cha dola za Kimarekani 2,500 kiasi cha Sh. Milioni 6.
    Kakamega Homeboys sasa watakutana na Simba katika Nusu Fainali Juni 7, na Nusu Fainali ya pili itaikutanisha Gor Mahia na mshindi kati ya AFC Leopards na Singida United zinazomenyana kesho.
    Na fainali ya michuano ya SportPesa Super Cup 2018 itafanyika Juni 10 na mshindi pamoja na kupata dola za Kimarekani 30,000 pia atapata nafasi ya kwenda kucheza na klabu ya Everton Uwanja wa Goodison Park mjini Liverpool, England. 
    Mshindi wa pili atajipatia dola za Kimarekani 10,000, wa tatu dola 7, 500 na wa nne dola 5,000 wakati timu nyingine zitapewa kifuta jasho cha dola 2,500. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAIFUTIA AIBU TANZANIA, YATINGA NUSU FAINALI SPORTPESA SUPER CUP Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top