• HABARI MPYA

    Friday, June 15, 2018

    SAMATTA AMUONGEZEA BANDA ‘HASIRA’ ZA KWENDA KUKIPIGA ULAYA

    Na Sada Salmin, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kimataifa wa Tanzania, Abdi Hassan Banda yuko Afrika Kusini anacheza soka ya kulipwa klabu ya Baroka FC, lakini hesabu zake ni kwenda Ulaya.
    Banda amethibitisha hayo baada ya kupewa zawadi ya jezi na mchezaji mwenzake wa Taifa Stars, Nahodha Mbwana Ally Samatta anayechezea klabu ya KRC Genk ya Ligi Kuu ya Ubelgiji.
    Samatta amemzawadia Banda jezi yake ya klabu ya Genk wiki iliyopita baada ya wote kukutana Dar es Salaam kwa mapumziko ya baada ya msimu.
    Abdi Banda akiwa amevaa jezi ya KRC Genk aliyopewa na Nahodha wake Taifa Stars, Mbwana Samatta 

    Na baada ya kupewa jezi hiyo, Banda ambaye kama Samatta wote wametokea klabu ya Simba ya Dar es Salaam, akaenda kuandika kwenye ukurasa wake wa Instagram; “Asante kaka @samagoal77 sumu hii ngoja nilale niote nipo huko,”.
    Banda anamaanisha jezi hiyo itamfanya aote naye yuko Ulaya, hivyo kuongeza juhudi katika klabu yake Baroka ili atimize ndoto za kufuata nyayo za Nahodha wake. 
    Mbwana Samatta (kulia) akiichezea klabu yake, KRC Genk nchini Ubelgiji

    Wiki iliyopita, wawili hao walikutana katika mechi ya hisani ya kuchangia madawati na ujenzi wa vyoo vya shule za msingi Dar es Salaam baina ya Samatta na Rafiki zake dhidi ya mwanamuziki Ally Kiba na Rafiki zake Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Katika mchezo huo uliofanyika Juni 9 na kuhushuriwa na Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe Team Samatta ilitoka nyuma kwa 2-0 na kushinda 4-2.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AMUONGEZEA BANDA ‘HASIRA’ ZA KWENDA KUKIPIGA ULAYA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top