• HABARI MPYA

    Saturday, March 03, 2018

    NJOMBE MJI FC YAIPIGA RUVU SHOOTING NA KUJINASUA MKIANI LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, NJOMBE
    TIMU ya Njombe Mji FC imefanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ruvu Shooting katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Saba Saba mjini Njombe.
    Katika mchezo huo ulioanza Saa 8:00 mchana, Njombe Mji walianza kupata bao dakika ya 27 kupitia kwa Nahodha wake, Ditram Nchimbi, kabla ya Baraka Mtuwi kuisawazishia Ruvu Shooting dakika ya 32.
    Kipindi cha pili, Jimmy Mwasomola akawainua wapenzi na mashabiki wa Njombe Mji FC waliojhitokeza Uwanja wa Saba Saba ulio kwenye eneo la Shule kadhaa za Msingi kwa kufunga bao la ushindi dakika ya 56.
    Ushindi huo, unaifanya Njombe Mji FC ifikishe pointi 18 baada ya kucheza mechi 20 na kujiondoa mkiani mwa Ligi Kuu ikipanda hadi nafasi ya 14.
    Lakini Njombe inaweza kukaa hapo kwa muda mfupi tu, kabla ya matokeo ya mechi kati ya Kagera Sugar na Maji Maji jioni hii Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba ambayo yanaweza kuwarudisha chini.
    Kagera Sugar na Maji Maji FC ya Songea mkoani Ruvuma zimeingia kwenye mechi ya 20 leo kila timu ikiwa na pointi 15.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo ni kati ya Tanzania Prisons na  Mbao FC inayoendelea hivi sasa na Azam FC dhidi ya Singida United itakayofuatia baadaye Saa 1:00 usiku. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NJOMBE MJI FC YAIPIGA RUVU SHOOTING NA KUJINASUA MKIANI LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top