• HABARI MPYA

    Saturday, March 17, 2018

    MTIBWA SUGAR WASEMA AZAM FC SAIZI YAO ROBO FAINALI ASFC, KAZI IPO MACHI 31 CHAMAZI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mkuu wa Mtibwa Sugar, Zuberi Katwila amesema maandalizi yao wanayofanya kuelekea mechi ya Robo Fainali ya Azam Sports Federation (ASFC) dhidi ya Azam FC ni kawaida akiamini kwamba viwango vyao viko sawa.
    Mtibwa na Azam zinatarajia kukutana kwenye mechi ya robo fainali ya michuano hiyo katika Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam, Machi 31, mwaka huu.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports - Online, Katwila alisema maandalizi yao yapo vizuri na kutohofia kiwango cha wapinzani wao hao kutokana na kulingana na aina ya viwango vinavyoonyeshwa na wachezaji wa Azam kulingana na wachezaji wake.
    Alisema kwa kutambua uzito wa mechi hiyo, hajatoa mapumziko yoyote kwa wachezaji wake  zaidi ya wale waliokwenda kujiunga na timu ya taifa na wanajifua kila siku.
    Kocha wa Mtibwa Sugar, Zuberi Katwila amesema Azam FC no sawa yao 

    “Hakuna mechi rahisi, pia sina hofu kabisa na Azam kwani nimewahi kukutana nao mara kadhaa nafahamu uchezaji wa wachezaji wake, kikubwa ni kuhakikisha vijana wangu wanakuwa makini katika maandalizi yetu kupata ushindi na kusonga hatua inayofuata,” alisema Katwila.
    Kwa upande wake, Kocha Msaidizi wa Azam FC, Idd Nassoro  Cheche, amesema wanakiandaa kikosi chake kuhakikisha wanamaliza kazi ndani ya dakika 90 katika mchezo wa kombe la Shirikisho dhidi ya Mtibwa Sugar.
    “Tunafanyia kazi mapungufu tuliyokuwa nayo kidogo kwenye mechi zetu za ligi tulizocheza huko nyuma, kurekebisha makosa, kuangalia kitu gani cha kufanya, kuiangalia Mtibwa uzuri wake na udhaifu wake ili tuandae vijana wetu wahakikishe tunakwenda kuwaangamiza Mtibwa,” alisema.
    Cheche alisema huo ni mchezo wa mtoano, lazima mmoja afungwe kama watatoka sare, kucheza  hatua ya penalti , hali hiyo wanahakikisha mchezo huo wanamaliza ndani ya  dakika 90.
    “Kikubwa ni kuanza kuwajenga wachezaji wetu mazoezini kwa sababu mazoezi ndiyo yatatupelekea kufanya vizuri huu mchezo kwa hiyo tuko makini kuhakikisha watu wanafanya mazoezi vizuri ili mechi iweze kuwa nyepesi kwetu,” alisema Cheche.
    Msimu uliopita timu hizo zilikutana kwenye hatua ya 16 bora ya michuano hiyo, mchezo ulifanyika kwenye Uwanja wa Azam Complex saa 10.00 jioni na Azam FC ikafanikiwa kuibuka kidedea kwa ushindi wa bao 1-0, liliwekwa kimiani na Ramadhan Singano ‘Messi’, akiunganisha pasi safi ya kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR WASEMA AZAM FC SAIZI YAO ROBO FAINALI ASFC, KAZI IPO MACHI 31 CHAMAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top