• HABARI MPYA

    Thursday, March 08, 2018

    MECHI YA SIMBA NA NJOMBE MJI YAAHIRISHWA, KESHO NI YANGA NA KAGERA SUGAR TAIFA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BODI ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeusogeza mbele mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baina ya wenyeji Njombe Mji FC na Simba SC uliopangwa kufanyika Jumapili Uwanja wa Saba Saba mjini Njombe.
    Hiyo inafuatia klabu ya Simba kuomba mchezo huo uahirishwe ili wapate fursa nzuri ya maandalizi kwa ajili ya mchezo wake wa marudiano Raundi ya Kwanza Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Al Masry mjini Cairo wiki ijayo.
    Simba inatarajiwa kumenyana na Al Masry Machi 17 mjini Cairo baada ya jana timu hizo kutoa sare ya 2-2 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Simba SC sasa hawatakwenda Njombe kucheza na Njombe Mji FC Jumapili ili wapate fursa ya kujiandaa vizuri na mechi dhidi ya Al Masry


    Wakiwa wanahitaji ushindi wa 1-0 ugenini ili kusonga mbele, Simba SC wameonekana kuelekeza nguvu zao kwenye maandalizi mazuri ili watimize malengo yao.
    Wakati huo huo; Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inatarajiwa kuendelea kesho kwa mchezo mmoja tu, mabingwa watetezi, Yanga SC wakiwakaribisha Kagera Sugar Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Pamoja na kwamba Yanga nayo inakabiliwa na mchezo wa marudiano wa Raundi ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Township Rollers ya Botswana Machi 17 tena baada ya kufungwa 2-1 kwenye mchezo wa kwanza juzi, lakini hawahitaji kuahirishiwa mechi za Ligi Kuu ya hapa.
    Yanga SC wao watatakiwa kushinda 2-0 ugenini wiki ijayo ili kuingia hatuan ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika – jambo ambalo ni gumu na kwa hali halisi ndani ya klabu hiyo wanaonekana kama wamekata tamaa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MECHI YA SIMBA NA NJOMBE MJI YAAHIRISHWA, KESHO NI YANGA NA KAGERA SUGAR TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top