• HABARI MPYA

    Friday, March 09, 2018

    BENCHI LA UFUNDI HALIJAFURAHIA YANGA KUCHEZA MECHI YOYOTE KABLA YA KURUDIANA NA TOWNSHIP ROLLERS

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BENCHI la Ufundi la Yanga SC halijafurahia timu kucheza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kabla ya kurudiana na Township Rollers katika Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Yanga wanatarajiwa kuteremka dimbani Saa 10:00 jioni ya leo kumenyana na Kagera Sugar katika mfululizo wa Ligi Kuu na Jumatatu watacheza na Stand United, mechi zote Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.
    Hiyo ni baada ya Jumanne kufungwa mabao 2-1 na Township Rollers ya Botswana katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Benchi la Ufundi Yanga; Kutoka kulia Meneja Hafidh Saleh, Kocha Msaidizi, Noel Mwandila, Kocha Mkuu George Mwandila na Kocha Msaidizi, Nsajigwa Shadrack

    Bin Zubeiry Sports – Online inafahamu benchi la Ufundi la Yanga chini ya Koch Mkuu, George Lwandamina limelalamikia ratiba hiyo inawanyima nafasi ya kuwandaa wachezaji kwa mechi ya marudiano na Rollers ambayo wanatakiwa kwenda kushinda 2-0 ugenini.
    Lakini inaonekana hakuna mawasiliano kati ya uongozi wa juu na benchi la Ufundi Yanga zaidi ya kupeana maagizo tu ndiyo maana leo timu inaingia kwenye mechi na Kagrea na Jumatatu itacheza na Stand United.
    Wakati huo huo, inafahamika morali ya wachezaji ndani ya timu ipo chini kutokana na kutolipwa mishahara yao kwa miezi mitatu sasa, wakati benchi la Ufundi nao hawajalipwa kwa zaidi ya miezi sita.
    Haijulikani chanzo cha hali ngumu ya kiuchumi ndani ya Yanga ni nini kwa sababu klabu ina wadhamini wasiopungua wanne, SportPesa, Macron, Azam TV na Maji ya Afya wakati huo huo inapata mgawo wa udhamini wa ushiriki wa Ligi Kuu kutoka Vodacom na malipo ya matangazo ya Televisheni kutoka Azam TV pamoja na fedha za ushiriki wa Azam Sports Federation Cup (ASFC).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BENCHI LA UFUNDI HALIJAFURAHIA YANGA KUCHEZA MECHI YOYOTE KABLA YA KURUDIANA NA TOWNSHIP ROLLERS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top