• HABARI MPYA

    Tuesday, January 02, 2018

    SIMBA SC YAANZA KWA SARE MAPINDUZI, SINGIDA UNITED YASHINDA 3-2

    Na Salum Vuai, ZANZIBAR
    SIMBA SC imelazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na Mwenge SC ya Pemba katika mchezo wake wa kwanza wa Kundi A, Kombe la Mapinduzi jioni ya leo Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Rashid Farahani aliyesaidiwa na Ali Ramadhani na Suleiman Karim, mabao yote yalipatikana kipindi cha kwanza.
    Iliwachukua dakika mbili tu Simba kupata bao la kuongoza kupitia kwa beki aliyechezeshwa kwenye nafasi yake ya zamani, kiungo Jamal Mwambeleko aliyemalizia kwa kichwa krosi ya beki wa kushoto, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’. 
    Mwenge wakasawazisha bao hilo dakika ya 28 kupitia kwa mshambuliaji wao, Humud Abdulrahman Ali aliyefumua shuti baada ya pasi ya Seif Pima Ame.
    Mshambuliaji John Bocco aliingia kipindi cha pili, lakini akashindwa kufunga Simba ikitoa sare ya 1-1 na Mwenge

    Pamoja na timu zote kufanya mabadiliko kipindi cha pili, lakini kupatikana kwa mabao mengine ilishindikana.
    Katika mchezo uliotangulia leo wa Kundi B, Singida United imeibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Zimamoto hapo hapo Amaan. Mabao ya Singida yamefungwa na Deus Kaseke dakika ya saba, Dany Usengimana dakika ya 21 na Kigi Makasi dakika ya 81, wakati ya Zimamoto yamefungwa na Ibrahim Hamad Ahmada ‘Hilika’ katika daika ya 39 na 84.
    Mechi nyingine ya Kundi B kati ya Yanga SC na Mlandege itafuatia Saa 2:15 usiku Uwanja wa Amaan pia.
    Kikosi cha Mwenge SC kilikuwa; Mudathir Khamis Mohammed, Omar Khatib Hamad, William Venence Michael, Yussuf Said Bwanga, Broklyn Bruno Costa, Hassan Ibrahim, Humoud Abrahman Ali, Mustanji Mussa Mustanji, Seif Pima Ame/Feisal Khamis Juma dk92, Ali Hamad Said/Juma Omar dk52 na Kambu Zubeir Zinyori. 
    Simba SC; Emanuel Mseja, Paul Bukaba, Mohamed Hussein ‘Tshabalala’, Yusuph Mlipili, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Ally Shomari/Kelvin Faru dk60, Said Hamisi, Juma Luizio/John Bocco dk46, Moses Kitandu/Nicholas Gyan dk46 na Jamal Mwambeleko/Shiza Kichuya dk46.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAANZA KWA SARE MAPINDUZI, SINGIDA UNITED YASHINDA 3-2 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top