• HABARI MPYA

    Monday, January 08, 2018

    SIMBA KATIKA MTIHANI MGUMU KOMBE LA MAPINDUZI LEO, YANGA…

    Na Salum Vuai, ZANZIBAR
    HATUA ya makundi za Kombe la Mapinduzi 2018 inahitimishwa leo kwa mechi mbili, vigogo Simba na Yanga wakimenyana na URA na Singida United.
    Simba SC wataanza kupambana na timu ya Mamlaka ya Mapato Uganda (URA) Saa 10:30 jioni kabla ya Yanga SC kumenyana na Singida United kuanzia Saa 2:15 usiku, mechi zote zikipigwa Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Yanga na Singida wamekwishafuzu Nusu Fainali na leo watakuwa wanapambana kuwania uongozi wa Kundi B baada ya wote kushinda mechi zao zote nne za awali.
    Simba wanatakiwa kuifunga URA leo Uwanja wa Amaan, Zanzibar ili kufuzu Nusu Fainali Kombe la Mapinduzi

    Lakini Simba na URA watakuwa katika mechi kali kweli, kila timu ikihitaji lazima ushindi ili kuungana na vinara wa Kundi A, Azam FC ambao pia ndiyo mabingwa watetezi kwenda Nusu Fainali.
    Kuelekea mchezo huo, URA inashika nafasi ya pili kwa pointi zake saba, nyuma ya Azam yenye pointi tisa, wakati Simba ni ya tatu kwa pointi zake nne.
    Maana yake Wekundu wa Msimbazi wanahitaji lazima ushindi ili kufuzu Nusu Fainali, tena kwa wastani wa mabao mbele ya URA ambayo leo itahitaji sare tu kusonga mbele.
    Ugumu wa mechi ya pili utategemea na matokeo ya mechi ya kwanza – kwa sababu hapana shaka zote Singida na Yanga zitachagua kupigania ushindi, au la kulingana na mpinzani wa Nusu Fainali wanayemtaka.
    Mechi ya URA na Simba itaamua timu gani itacheza na timu gani katika Nusu Fainali, kwani Mshindi wa kwanza wa Kundi A atamenyana na Mshindi wa Pili wa Kundi B na Mshindi wa pili wa Kundi B atamenyana na Mshindi wa Pili wa Kundi A mechi hizo zikipigwa Jumatano na Fainali itafuatia Jumamosi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA KATIKA MTIHANI MGUMU KOMBE LA MAPINDUZI LEO, YANGA… Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top