• HABARI MPYA

    Wednesday, January 17, 2018

    OKWI AWAOMBA MSAMAHA WACHEZAJI WENZAKE, MAKOCHA SIMBA SC

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    KAIMU Kocha Mkuu wa Simba SC, Masoud Juma amesema kwamba mshambuliaji Emmanuel Okwi ameomba msamaha kwa kuchelewa kujiunga na timu kufuatia ruhusa maalum aliyopewa.
    Akizungumza mjini Morogoro baada ya mazoezi ya leo asubuhi, Juma ambaye ni raia wa Burundi amesema kwamba Okwi amekwishajiunga na timu na ameomba radhi kwe wenzake. 
    “Okwi alikuja akaomba samahani kwa wachezaji na watu wote. Unajua binadamu kila mtu hakuna aliyekamilika, muhimu ni kuungana kwa pamoja bila kunyoosheana vidole,”amesema.
    Emmanuel Okwi ameomba msamaha kwa kuchelewa kujiunga na timu kufuatia ruhusa maalum aliyopewa

    Aidha, Juma amesema kwamba wamekuwa na wiki nzuri ya maandalizi katika kambi yao ya Morogoro kujiandaa na mchezo wao wa kesho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Singida United Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam. 
    Amesema baada ya kambi hiyo sasa wanarejea Dar es Salaam kwa matarajio ya kufanya vizuri kwenye mchezo wao huo wa kesho.
    Simba SC inaongoza Ligi Kuu kwa sasa kwa pointi zake 26 baada ya kucheza mechi 12, ikiwa sawa kabisa na Azam FC na inawazidi kwa pointi tatu Singida United na pointi tano mabingwa watetezi, Yanga SC.
    Yanga wanateremka dimbani leo Uwanja wa Uhuru kumenyana na Mwadui FC ya Shinyanga wakati Azam FC watakuwa wageni wa Maji Maji kesho Uwanja wa Maji Maji mjini Songea katika mechi ya kukamilisha raundi ya 13 ya Ligi Kuu. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OKWI AWAOMBA MSAMAHA WACHEZAJI WENZAKE, MAKOCHA SIMBA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top