• HABARI MPYA

    Tuesday, January 02, 2018

    MFARANSA NDIYE KOCHA MPYA WA UGANDA THE CRANES

    MFARANSA Sebastien Desabre ameteuliwa kuwa kocha mpya wa timu ya taifa ya Uganda na kusaini mkataba wa miaka mitatu.
    Anachukua nafasi ya Mserbia, Milutin Micho Sredejovic ambaye alijiuzulu miezi michache iliyopita na kujiunga na vigogo wa Afrika Kusini, Orlando Pirates.
    Desabre hivi karibuni alikuwa anafundisha klabu ya Ismailia ya Misri na alitambulishwa katika tafrija fupi iliyofanyika mjini Kampala Alhamisi ya Desemba 28 mwaka 2017 baada ya kufikia makubaliano na Shirikisho la Soka Uganda (FUFA).
    Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya FUFA, Hamid Juma (kushoto) akimkabidhi jezi ya The Cranes, kocha mpya wa Uganda, Sebastien Desabre. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa FUFA, Edgar Watson

    "Desabre amewashinda makocha wengine 93 walioomba nafasi na sasa atakuwa Kocha Mkuu wa timu zote za taifa (zikiwemo za vijana za U-23, U-20 na U-17) kwa sababu falsafa ya FUFA ni kujenga timu ya taifa kutokea chini” amesema Mtendaji Mkuu wa FUFA, Edgar Watson.
    Desabre atasaidiwa na Mathias Lule, alikuwa Msaidizi wa kocha wa muda, Moses Basena.
    "Nina furaha kuwa hapa na nitajaribu bahati yangu kwa kufanya bidii ya kazi nzuri na kuwafurahisha mamilioni ya Waganda. Nimekuwa nikiifuatilia Uganda na sasa nawajua baadhi ya wachezaji,".
    “Uganda ni taifa kubwa kisoka na sasa kazi iliyopo mbele ni kujiandaa kwa michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) na hatuna muda zaidi ya kuanza kumulika michuano iliyopo mbele yetu,” alisema Desabre kuwaambia Waandishi wa Habari.
    Kocha huyo mwenye umri wa miaka 41 baadhi ya timu alizofundisha ni pamoja na ASEC Mimosas ya Ivory Coast, Coton Sport Garoua ya Cameroon, Wydad Athletic Club ya Morocco na Esperance ya Tunisia.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MFARANSA NDIYE KOCHA MPYA WA UGANDA THE CRANES Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top