• HABARI MPYA

    Friday, January 05, 2018

    MAREFA WATATU WAFUNGIWA MIAKA MITATU KUVURUNDA MECHI YA DODOMA FC V ALLIANCE FC

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MAREFA wote wanne waliochezesha mechi namba 39 ya Kundi C Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara kati ya Dodoma FC iliyoshinda 3-2 dhidi ya Alliance Schools wamefungiwa kwa kuchezesha chini ya kiwango.
    Hayo yamefikiwa katika kikao cha Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi, maarufu Kamati ya Saa 72 kilichofanyika jana mjini Dar es Salaam kujadili mechi mbalimbali za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Ligi Daraja la Kwanza na Daraja la Pili.
    Waamuzi waliofungiwa ni Andrew Shamba, Abdallah Mkomwa, Athuman Athuman na Omari Juma ambao kila mmoja atatumikia kifungo cha miaka mitatu kwa mujibu wa Kanuni ya 38(1a) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Udhibiti wa Waamuzi.
    Andrew Shamba akizongwa na wachezaji wa Yanga miaka sita ilitopita kwa maamuzi yake ya utata

    Kamisaa wa mechi hiyo Mackshem T. Nzunda naye amefungiwa miaka mitatu kwa kushindwa kutoa taarifa ya mchezo kwa usahihi. Adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 39(1) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Udhibiti wa Kamishna.
    Kamati imeomba suala la waamuzi hao ambao baadhi yao ni wa Ligi Kuu, kupitia TFF liwasilishwe kwenye chombo chenye dhamana ya kisheria ya rushwa kufanyiwa uchunguzi zaidi.
    Pamoja na hayo, Klabu ya Alliance Schools imepigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) kwa timu yake kuonyeshwa kadi zaidi ya tano katika mechi hiyo iliyofanyika Desemba 30, 2017 mjini Dodoma. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42 (10) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Udhibiti wa Klabu.
    Mchezaji Shaban William wa Alliance Schools amesimamishwa, hadi suala lake la kumpiga Mwamuzi litakaposikilizwa na Kamati ya Nidhamu ya TFF. Uamuzi wa kumsimamisha umezingatia Kanuni ya 9(5) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Usimamizi wa Ligi.
    Katika hatua nyingine, Mufindi United imepigwa faini ya Sh. 500,000 kutokana na kiongozi wake, Hussein Turuka kutoa lugha chafu kwa mwamuzi katika mechi namba 37 ya Kundi B dhidi ya JKT Mlale iliyoshinda 1-0 Desemba 31, 2017 mjini Songea. Adhabu hiyo imezingatia Kanuni ya 42(1) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Udhibiti wa Klabu.
    Mawenzi Market imepigwa faini ya Sh. 500,000 baada ya mashabiki wake kutaka kuwapiga waamuzi na kuwashawishi vijana waokota mipira kuchukua mipira iliyotoka nje na kuipeleka jukwaani katika mechi namba 40 wakishinda 1-0 dhidi ya Polisi Dar Desemba 31, 2017. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42(1) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Udhibiti wa Klabu.
    Kocha Mkuu wa Mawenzi Market amepewa Onyo Kali kwa kuchelewa kwenye kikao cha maandalizi ya mechi (pre-macth meeting) kwa dakika saba. Adhabu hiyo imezingatia Kanuni ya 14(3) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Taratibu za Mchezo. MECHI YA MVUVUMWA VS FRIENDS RANGERS
    Kamati imeipa Friends Rangers ushindi wa pointi tatu na mabao matatu baada ya Mvuvumwa kuchezesha wachezaji ambao hawajasajiliwa (non qualified) katika mechi ya Kundi A Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kati ya timu hizo iliyochezwa Oktoba 29, 2017. Mvuvumwa ilishinda mechi hiyo mabao 4-1.
    Uamuzi huo dhidi ya Mvuvumwa umefanywa kwa kuzingatia Kanuni ya 14(18) na 42(20) za Ligi Daraja la Kwanza. Nayo Friends Rangers imepewa ushindi kwa kuzingatia Kanuni ya 14(37) na ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Taratibu za Mchezo.  
    Vilevile viongozi wa Mvuvumwa waliohusika kughushi leseni zilizotumiwa na wachezaji hao ambao hawakusajiliwa watafikishwa kwenye Kamati ya Maadili ya TFF kwa ajili ya hatua zaidi.
    Kamati imepitia malalamiko ya Alliance Schools kupinga uchezeshaji wa Mwamuzi wa mechi yao dhidi ya Dodoma FC iliyofanyika Desemba 30, 2017 Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.
    Baada ya kupitia hoja zote, Kamati haikukubaliani na malalamiko hayo kwa vile hayakuwa na vielelezo wala kanuni za kuyathibitisha. Pia kwa suala la muda, Kamati imejiridhisha kuwa kazi ya kutunza muda ni ya Mwamuzi.
    Katika Ligi Daraja la Pili;  Mechi namba 18 Kundi B (Africans Sports 1 v Kitayosce 2). Kitayosce imepigwa faini ya sh. 50,000 (elfu hamsini) baada ya kuhudhuria kikao cha maandalizi ya mechi (pre-match meeting) ikiwa na maofisa watatu badala ya wanne, hivyo kwenda kinyume na Kanuni ya 14(2b) ya Ligi Daraja la Pili kuhusu Taratibu za Mchezo.
    Adhabu dhidi yao katika mechi hiyo iliyofanyika Desemba 29, 2017 jijini Tanga imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 14(3) ya Ligi Daraja la Pili kuhusu taratibu za Mchezo.
    Mechi namba 16 Kundi C (Mighty Elephant 1 v Green Warriors 3). Kocha wa Green Warriors, Azish Kondo amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) baada ya kuondolewa kwenye mchezo (ordered off) na Mwamuzi kwa kutumia lugha chafu.
    Adhabu hiyo dhidi ya Kocha Kondo katika mechi hiyo iliyofanyika Desemba 29, 2017 mjini Songea imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 40(10) ya Ligi Daraja la Pili kuhusu Udhibiti wa Makocha.
    Mechi namba 18 Kundi C (Mkamba Rangers 0 v Boma 1). Klabu ya Mkamba Rangers imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kutokana na washabiki wake kuingia uwanjani (pitch).  Adhabu hiyo katika mechi hiyo iliyochezwa Desemba 29, 2017 ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42(1) ya Ligi Daraja la Pili kuhusu Udhibiti wa Klabu.
    Mechi namba 16 Kundi D (Area C v Nyanza). Timu ya Nyanza FC imeshushwa madaraja mawili na matokeo ya michezo yako yote imefutwa kwa kutofika uwanjani bila kutoa sababu yoyote na kusababisha mechi yao dhidi ya Area C iliyokuwa ichezwe Desemba 29, 2017 mjini Dodoma isifanyike.
    Uamuzi huo dhidi ya Nyanza FC umefanywa kwa kuzingatia Kanuni ya 28(1) ya Ligi Daraja la Pili kuhusu Kutofika Uwanjani. Pia kwa mujibu wa Kanuni ya 28(2) ya Ligi Daraja la Pili kuhusu Kutofika Uwanjani, imepigwa faini ya sh. 2,000,000 (milioni mbili) ambapo sh. 1,000,000 (milioni moja) itachukuliwa na Bodi ya Ligi, na sh. 1,000,000 (milioni moja) italipwa timu pinzani.
    Vilevile Kamati imeiomba Sekretarieti kukiandikia barua Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Manyara (MARFA) ili kujua tatizo la timu hiyo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAREFA WATATU WAFUNGIWA MIAKA MITATU KUVURUNDA MECHI YA DODOMA FC V ALLIANCE FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top