• HABARI MPYA

    Friday, January 05, 2018

    JKT RUVU YABADILISHWA JINA TENA, SASA YAITWA JKT TANZANIA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya JKT Ruvu inayoshiriki Ligi Daraja La Kwanza Tanzania Bara Kundi A msimu huu, sasa itajulikana kwa jina la JKT Tanzania SC.
    Taarifa ya Msemaji wa timu, Afisa Mteule Daraja la Pili, Costantine Masanja, imesema kwamba JKT Tanzania ndiyo imepitishwa kuwa timu pekee inayomililikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa itakayobaki kwenye usajili wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
    Hiyo ni kufuatia TFF kuamua kutilia mkazo agizo la Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) juu ya mmiliki mmoja kutokuwa na timu zaidi ya moja katika ligi za nchi na Masanja amesema maskani ya JKT Tanzania yataendelea kuwa makao makuu ya jeshi hilo, Mlalakuwa.
    “Mababadiliko haya yamekuja baada baada ya kupata maelekezo kutoka bodi ya ligi kwa taasisi kumiliki timu moja, taratibu zote zimefuatwa katika kutekeleza agizo hili, uongozi wa JKT Ruvu unatoa shukrani za dhati kwa Bodi Ya Ligi na TFF kwa ushirikiano mkubwa walioutoa kupitia mamlaka/idara zake wakati wa mchakato mzima kuhusu suala hili muhimu kwa ustawi wa taifa letu kupitia mpira wa miguu,”amesema.
    Aidha, Masanja amesema Mwenyekiti wa JKT Ruvu, Luteni Kanali Hassan Mabena alikwishatolea ufafanuzi wa kina suala hilo kupitia baadhi ya vyombo vya habari.
    JKT Tanzania kwa sasa ipo kambini na inaendelelea na mazoezi katika Uwanja wa Meja Jenerali Michael Isamuhyo, Mbweni JKT, chini ya kocha wake Mkuu, Bakari Shime, tayari kwa mchezo wake na Mvuvumwa FC Januari 13 Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
    Kocha Shime amedhamiria kuhakikisha timu yake inashinda michezo yote iliyobaki ili kutimiza malengo waliyojiwekea ya kurejea Ligi Kuu.
    Pamoja na kushiriki Ligi Daraja la Kwanza, JKT Tanzania pia ipo katika hatua ya 32 Bora ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) na imepangwa kucheza na Polisi Dar es Salaam.
    Historia ya JKT Tanzania inaanzia mwaka 1970 katika kambi ya JKT Mgulani mjini Dar es Salaam ilipoanzishwa kwa jina la JKT Kabambe, kabla ya mwaka 1973 kuhamishiwa katika kikosi cha Ruvu JKT mkoani Pwani na mwaka 1975 ikabadilishwa jina na kuitwa JKT Ruvu.
    Mwaka 1999 timu hiyo ilihamishiwa makao makuu ya Jeshi la Kujenga Taifa, Mlalakuwa mjini Dar es Salaam ingawa iliendelea kujulikana kama JKT Ruvuy hadi Desemba 12, mwaka jana ilipobadilishwa tena jina na kuwa JKT Tanzania.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JKT RUVU YABADILISHWA JINA TENA, SASA YAITWA JKT TANZANIA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top