• HABARI MPYA

    Thursday, December 14, 2017

    ZANZIBAR KUMKOSA MWINYI MNGWALI KESHO DHIDI YA UGANDA CHALLENGE

    Na Mwandishi Wetu, KISUMU
    BEKI wa kushoto, Mwinyi Hajji Mngwali atakosekana kwenye kikosi cha Zanzibar kesho katika mchezo wa Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge dhidi ya mabingwa watetezi, Uganda.
    Zanzibar Heroes watakipiga na Uganda katika mchezo wa nusu fainali ya pili kwenye mashindano ya CECAFA Challenge, mchezo utakaopigwa Saa 9:00 Alasiri Uwanja wa Moi mjini Kisumu, Kenya.
    Mwinyi ataukosa mchezo huo mara baada ya kupigwa kadi mbili za njano katika michezo miwili mfululizo iliyopita ukiwepo waliotoka sare ya 0-0 na Kenya na ule waliofungwa 1-0 na Libya ambapo kanuni ya mashindano hayo mchezaji akipewa kadi mbili mfululizo za njano katika michezo miwili mfululizo atalazimika kuukosa mchezo unaofuata.
    Mwinyi Hajji Mngwali atakosekana kwenye kikosi cha Zanzibar kesho Uganda

    Nafasi ya Mwinyi kesho itazibwa na Adeyum Ahmed Seif ambae pia ni mzoefu katika Mashindano hayo ya Cecafa.
    Mbali ya Mwinyi pia Zanzibar Heroes itawakosa huduma za nyota wake wengine akiwepo mfungaji wao Kassim Suleiman Khamis pamoja na kiungo Amour Suleiman “Pwina” ambao wote ni majeruhi.
     “Mwinyi hatocheza ana kadi 2 za njano, lakini pia Kassim na Amour nao tutawakosa kutokana na majeruhi”. Alisema Kocha wa Zanzibar Heroes Hemed Suleiman (Morocco).
    Lakini kwa upande wa timu ya Uganda kesho itawakosa nyota wake wawili muhimu akiwemo Mulema Isaack na Awany Tinoethy ambao wote walipewa kadi mbili za manjano katika michezo miwili mfululizo iliyopita.
    "Ni mechi ngumu nawajua sana Zanzibar lakini na sisi tutawaonyesha kama tunataka kulitetea kombe letu". Alisema Moses Basena kocha mkuu wa Uganda.
    Morocco ametaja kikosi chake kitakachocheza ambacho ni; Mohammed Abulrahman Mohamed ‘Wawesha’, Ibrahim Mohamed Said ‘Sangula’, Adeyum Ahmed Seif, Abdullah Salum Kheri ‘Sebo’, Issa Haidari Dau ‘Mwalala’, Abdulaziz Makame Hassan ‘Abui’, Mohamed Issa Juma ‘Banka’, Mudathir Yahya Abass, Ibrahim Hamad Ahmada ‘Hilika’, Feisal Salum Abdallah ‘Fei Toto’ na Suleiman Kassim Suleiman ‘Seleembe’, ambaye ni Nahodha.
    Katika benchi watakuwapo Ahmed Ali Suleiman ‘Salula’, Nassor Mrisho Salim, Mohamed Othman Mmanga, Ibrahim Abdallah Hamad, Abdullah Haji Shaibu ‘Ninja’, Seif Abdallah Rashid ‘Karihe’, Hamad Mshamata Makame, Khamis Mussa Makame ‘Rais’ na Abdul swamad Kassim Ali ‘Hasgut’.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ZANZIBAR KUMKOSA MWINYI MNGWALI KESHO DHIDI YA UGANDA CHALLENGE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top