• HABARI MPYA

    Monday, December 11, 2017

    STARS ‘ALWAYS NEXT TIME’…ZANZIBAR KUKUTANA NA UGANDA NUSU FAINALI

    Na Mwandishi Wetu, MACHAKOS
    ZANZIBAR itakutana na mabingwa watetezi, Uganda katika mchezo wa Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge inayoendelea nchini Kenya, Desemba 15, mwaka huu.
    Hiyo itakuwa Nusu Fainali ya pili, baada ya Nusu Fainali ya kwanza kati ya wenyeji, Kenya dhidi ya Burundi Desemba 14.
    Na hiyo ni baada ya Kenya kuifunga 1-0 Tanzania Bara katika mchezo wa mwisho wa Kundi A jioni ya leo Uwanja wa Jomo Kenyatta, Kenya.  
    Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Alex Muhabi aliyesaidiwa na Dick Okello na Ronald Katenya, wote wa Uganda, bao pekee la Harambee Stars lilifungwa na Vincent Ouma dakika ya 19, akimalizia mpira uliotemwa na kipa Peter Manyika baada ya krosi ya Ochieng Ovella aliyempita kutoka kwa chenga ya hadi chenga beki Kennedy Wilson.
    Kilimanjaro Stars ya kocha Ammy Ninje ilifunguka na kuanza kupeleka mashambulizi langoni mwa Harambee kusaka bao la kusawazisha, lakini hawakufanikiwa. Kenya wanafikisha pointi nane na kumaliza juu ya kundi wakifuatiwa na Zanzibar waliomaliza na pointi saba. 
    Mechi nyingine ya Kundi A iliyotangulia mchana wa leo, Libya ilishinda 1-0 dhidi ya Zanzibar, bao pekee la Alharaish Zakaria dakika ya 24 Uwanja wa Jomo Kenyatta mjini Machakos, Kenya leo, wakati mchezo wa mwisho wa Kundi B, Burundi iligawana pointi na Sudan Kusini baada ya sare ya 0-0 Uwanja wa Bukhungu mjini Kakamega.
    Hiyo inamaanisha Uganda inamaliza kileleni mwa Kundi B kwa pointi zake tano sawa na washindi wa pili, Burundi ambao wanazidiwa wastani wa mabao.
    Kikosi cha Kenya kilikuwa; Matasi Patrick Musotsi, Nicholas Dennis Sikhayi, Atudo Jockins Otieno, Mayeko Musa Mohammed, Onguso Wesley Arasa, Omutiti Patilah Omoto, Kisia Ernst Wendo, Ogutu George Odhiambo, Ochieng Ovella/Samuel Onyango dk83, Ochieng Chrispin Ouma Na Oburu Vincent Ouma.
    Tanzania Bara; Peter Manyika, Himid Mao, Gardiel Michael, Kennedy Willson, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Abdul Hilal/Yohanna Nkomola, Hamisi Abdallah/Amani Kyatta, Daniel Lyanga, Ibrahim Ajib na Shiza Kichuya/Yahya Zayed.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STARS ‘ALWAYS NEXT TIME’…ZANZIBAR KUKUTANA NA UGANDA NUSU FAINALI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top