• HABARI MPYA

    Monday, December 11, 2017

    SALAH AWA MWANASOKA BORA WA AFRIKA WA BBC 2017

    MMISRI Mohamed Salah amechaguliwa kuwa Mwanasoka Bora wa Mwaka 2017 wa Afrika wa Shirika la Utangazaji Uingereza (BBC).
    Kufuatia kura nyingi za rekodi, nyota huyo wa Liverpool amewapiku Pierre-Emerick Aubameyang wa  Gabon,Naby Keita wa Guinea, Sadio Mane wa Senegal na Victor Moses wa Nigeria.
    "Nina furaha kushinda tuzo hii," amesema mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25.
    "Wakati wote ni hisia maalum unaposhinda kitu fulani. Nahisi kama nilikuwa nina mwaka mzuri, hivyo nina furaha sana,".
    Salah, anayeongoza kwa mabao katika Ligi Kuu ya England akiwa amefunga mara 13, amekuwa na mwaka mzuri kote, timu ya taifa na klabu.
    Mapema mwaka 2017, alitoa mchango mkubwa kwa Misri kushika nafasi ya pili kwenye Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
    Pia alishiriki kwenye kila bao kati ya yote saba yaliyowapeleka Mafarao Fainali za Kombe la Dunia mwakani kwa mara ya kwanza tangu 1990 - akisaidia mawili na kufunga matano, likiwemo la penalti ya dakika ya mwisho dhidi ya Kongo lililowapa tiketi ya Urusi.
    Nchini Italia, alifunga mabao 15 na kusaidia kupatikana kwa mengine 11 akiiwezesha Roma kumaliza nafasi ya pili kwenye Serie A, nafasi nzuri zaidi kwao kwao kwa miaka saba, kabla ya kujiunga na Liverpool ambako hadiu sasa amefunga mabao 13 katika mechi 16 za mwanzo za ligi.
    "Ningependa kuwashukuru wachezaji wenzangu wa Liverpool na pia nimekuwa na msimu mzuri na Roma, hivyo napaswa kuwashukuru wachezaji wenzangu huko na wachezaji wenzangu katika timu ya taifa,"alisema Salah.

    Mohamed Salah ndiye Mwanasoka Bora wa Mwaka 2017 wa Afrika wa BBC
    ORODHA YA WASHINDI WA TUZO 
    YA MWANASOKA WA BBC AFRKA
    2016: Riyad Mahrez (Leicester City & Algeria)
    2015: Yaya Toure (Manchester City & Ivory Coast)
    2014: Yacine Brahimi (Porto & Algeria)
    2013: Yaya Toure (Manchester City & Ivory Coast)
    2012: Chris Katongo (Henan Construction & Zambia)
    2011: Andre Ayew (Marseille & Ghana)
    2010: Asamoah Gyan (Sunderland & Ghana)
    2009: Didier Drogba (Chelsea & Ivory Coast)
    2008: Mohamed Aboutrika (Al Ahly & Misri)
    2007: Emmanuel Adebayor (Arsenal & Togo)
    2006: Michael Essien (Chelsea & Ghana)
    2005: Mohamed Barakat (Al Ahly & Misri)
    2004: Jay-Jay Okocha (Bolton & Nigeria)
    2003: Jay-Jay Okocha (Bolton & Nigeria)
    2002: El Hadji Diouf (Liverpool & Senegal)
    2001: Sammy Kuffour (Bayern Munich & Ghana)
    2000: Patrick Mboma (Parma & Cameroon)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SALAH AWA MWANASOKA BORA WA AFRIKA WA BBC 2017 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top