• HABARI MPYA

    Tuesday, December 12, 2017

    MTIBWA SUGAR WAISHANGAA ZFA KUWAENGUA KOMBE LA MAPINDUZI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Mtibwa Sugar imekishangaa Chama cha Soka Zanzibar (ZFA) kwa kutowajumuisha kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi la Mapinzuzi mwaka huu.
    Katibu Msaidizi wa Mtibwa, Abubakar Swabur ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba wanastaajabu kutojumuishwa kwenye Kombe wakati wao ni washiriki wazoefu na wa kihistoria. 
    “Sisi ni kati ya washiriki wa kwanza kabisa wa Kombe la Mapinduzi mwaka 2007 lilipoanzishwa na tumeendelea kushiriki bila kukosa wakati wote. Tumekuwa tukishiriki hata wakati ambao timu nyingine kubwa za Bara hazikutaka kwenda. Kwa kiasi kikubwa sisi tumeibeba sana ile michuanjo, ila ajabu leo tunawekwa kando,”amesema Swabur.
    Hata hivyo, Mtibwa wamesema hawana kinyongo na waandaaji wa michuano hiyo kwa sababu wao ndiyo wenye uamuzi. “Sisi tunaelekeza nguvu zetu kwenye majukumu yetu mengine, tunawaachia Mapinduzi yao, ila tunaipenda sana hiyo michuano,”amesema Swabur.
    Mtibwa Sugar ni kati ya waasisi wa Kombe la Mapinduzi mwaka 2007 na ilifika fainali ambako ilikutana na Yanga SC na kufungwa 2-1.
    Ilifika tena fainali mwaka 2008 ikafungwa na Simba, kabla ya kubeba taji lake pekee la michuano hiyo mwaka 2010 ikiifunga Ocean View katika fainali.
    Ikafanikiwa kucheza fainali mbili mfululizo mwaka 2015 ikifungwa na Simba SC na 2016 ikifungwa na  URA ya Uganda.
    Katika hatua nyingine, Swabur amesema kwamba makipa wao wawili waliokuwa majeruhi, Shaaban Kado na Abdallah Makangana wote wamepona na wamejiunga na timu Manungu, Turiani mkoani Morogoro kwa mazoezi. 
    Swabur amesema beki Dicksons Daudi anaendelea kupata ahueni ya maumivu ya jino taratibu akiwa kambini na akipona ataanza mazoezi.
    Ameongeza kwamba ni wachezaji wawili tu wanakosekana kwa sasa kambini Mtibwa Sugar, beki Salum Kanoni anayesumbuliwa na maumivu ya enka na kiungo Henry Hoseph anayeumwa goti.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR WAISHANGAA ZFA KUWAENGUA KOMBE LA MAPINDUZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top