• HABARI MPYA

    Sunday, December 03, 2017

    ‘MO’ DEWJI AAHIDI ‘SIMBA YA KIMATAIFA’ BAADA YA KUSHINDA ZABUNI YA HISA MSIMBAZI

    Na Salma Suleiman, DAR ES SALAAM
    MFANYABIASHARA Mohammed ‘Mo’ Dewji ameshinda zabuni ya uwekezaji kwenye klabu ya Simba SC ya Dar es Salaam.
    Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Uwekezaji, Jaji Mstaafu Thomas Mihayo katika Mkutano Mkuu Maalum wa Simba uliofanyika ukumbi wa Mwalimu Nyerere, Dar es Salaam.
    Mo pekee aliweka dau la Sh Bilioni 20 kuomba asilimia 50 ya hisa, baada ya klabu kutangaza kuuza asilimia 50 ya hisa zake kwa Sh. Bilioni 20 miezi miwili iliyopita, ingawa baadaye Serikali ikaagiza klabu hiyo isiuze zaidi ya asilimia 49 kwa mtu mmoja.
    Mohammed ‘Mo’ Dewji akishukuru baada ya kushinda zabuni ya uwekezaji Simba SC 

    Mohammed ‘Mo’ Dewji akishukuru baada ya kushinda zabuni ya uwekezaji Simba SC 

    Wanachama 1320 wamehudhuria mkutano huo kutoka Dar es Salaam na mikoa jirani na kwa furaha ya ushindi huo, Mo Dewji ametoa ahadi 10 za kuleta mabadiliko makubwa.
    Mo ameahidi katika mwaka wa kwanza wa uwekezaji wake, ataanza na ujenzi wa Uwanja wa mazoezi wa nyasi za asili na nyasi bandia pamoja na hosteli ya kisasa ya wachezaji.
    Amesema, hosteli hiyo itajengwa upya na itakuwa ya kisasa yenye vyumba 35, huku 30 kati ya hivyo vitakuwa kwa ajili ya wachezaji na vitano kwa ajili ya benchi la ufundi na kila kitu ndani.
    “Nimefurahi na ninashukuru Mungu kwani kutokana na matakwa yake ndiyo nimefanikisha jambo hili, lakini pia Kamati iliyosimamia mchakato huu kwa ujumla, wanachama na wapenzi wa klabu ya Simba kwa kukubali mabadiliko ya uendeshaji wa klabu,” amesema Mo.
    Aidha, Mo amesema Simba itakuwa na gym yake ya kisasa, bwawa kubwa la kuogelea kwa ajili ya mazoezi na sehemu ya kupumzika kwa wachezaji kukiwa Pool table na Play Station, mgahawa kwa ajili ya chakula cha wachezaji, kuanzisha kituo cha kukuzia vipaji kwa vijana akianza na wale wenye umri wa chini ya miaka 14, 16 na 18 na lengo ni kuwakuza.
    “Simba itaanza kufanya mambo kimataifa na kushindana na timu kubwa za Afrika kama TP Mazembe na Esperance pia kuitangaza na kuikuza bidhaa yake ikiwa ni pamoja na kutengeneza vifaa mbalimbali kama fulana, kofia, vishika ufunguo na kadhalika,” amesema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ‘MO’ DEWJI AAHIDI ‘SIMBA YA KIMATAIFA’ BAADA YA KUSHINDA ZABUNI YA HISA MSIMBAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top