• HABARI MPYA

    Wednesday, November 15, 2017

    NDIKUMAMA WA IRENE UWOYA AFARIKI DUNIA RWANDA

    Na Mwandishi Wetu, KIGALI
    BEKI wa zamani wa kimataifa wa Rwanda, Hamad Ndikumana ‘Katauti’ na mume wa kwanza wa msanii nyota wa filamu Tanzania, Irene Uwoya amefariki dunia usiku wa kuamkia leo.
    Habari zinasema Ndikumana amefariki mjini Kigali, Rwanda lakini huenda akasafirishwa kurudishwa nyumbani kwao kwa asili, Burundi. Pamoja na Ndikumana, taifa la Rwanda limepata misiba miwili jumla leo, kufuatia mchezaji mwingine wa zamani wa timu ya taifa na klabu ya Rayon pia, Hategekimana Bonaventura 'Gangi' naye kufariki dunia usiku wa kuamkia leo.
    Kwa upande wa Ndikumana, hadi anakutwa na umauti, alikuwa Kocha Msaidizi wa Rayon Sports chini ya kocha Mkuu, Olivier Karekezi ambaye alicheza naye The Blues enzi zake.
    Uongozi wa Rayon umesema Katauti alifanya mazoezi na wachezaji wake vizuri jana, lakini wakati wa kuondoka akasema anajisikia maumivu ya kifua na tumbo na asubuhi ya leo ndiyo imegundulika Ndikumana amefariki dunia na mwili wake umepelekwa katika chumba kuhifadhia maiti hospitali ya Rwampala.
    Hamad Ndikumana ‘Katauti’ akipunga mkono hivi karibuni wakati akichezea timu ya maveterani wa Rwanda 

    Na umauti unamkuta Ndikumana siku chache baada ya aliyekuwa mkewe, Irene Uwoya kuolewa na msanii kijana mdogo, Dogo Janja nchini Tanzania. 

    Ndikumana aliyezaliwa Oktoba 5, mwaka 1978, kisoka aliibukia kwao Burundi kabla ya kuhamia Kigali, Rwanda ambako alichezea Rayon kati ya mwaka 1998 na 1999 kabla ya kwenda Ubelgiji ambako alichezea timu za KV Turnhout 2000 hadi 2001 alipohamia RSC Anderlecht 2002 hadi 2003 alipojiunga na  KV Mechelen alikocheza hadi 2003 alipohamia KAA Gent alikocheza hadi 2005 alipohamia APOP Kinyras Peyias FC.
    Mwaka 2006 alihama nchi na kwenda Cyprus ambako alianza na klabu ya Nea Salamina hadi 2008 alipohamia Anorthosis Famagusta alikocheza hadi 2009 alipohamia AC Omonia alikocheza hadi 2010 alipohamia AEL Limassol ambako alidumu hadi 2011 aliporejea Ubelgiji kujiunga na APOP Kinyras Peyias FC, iliyokuwa klabu yake ya mwisho Ulaya.
    Hamadi Ndikumana enzi zake anacheza Ulaya alicheza michuano mikubwa hadi Ligi ya Mabingwa
    Hamadi Ndikumana wakati anachezea timu ya taifa ya Rwanda

    Mwaka 2012 alirudi Burundi kumalizia soka yake katika klabu ya Vital’O kama kocha mchezaji kabla ya m
    waka 2015 kwenda kusaini Stand United ya Shinyanga katika Ligi Kuu, ingawa hakudumu akarejea Rwanda kuanza rasmi kazi ya ukocha.
    Ndikumana alikuwa beki na Nahodha wa kikosi cha Rwanda, alichokichezea mechi
    50 kuanzia mwaka 1998 katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2004 nchini Tunisia, ambazo zilikuwa za kwanza na pekee hadisasa kwa Amavubi. 
    Marehemu ameacha watoto akiwemo mmoja aliyezaa na Uwoya ambaye anaishi na mama yake Dar es Salaam. 
    Mungu ampoumzishe kwa amani marehemu. Amin.

    Hamadi Ndikumana akiwa na mkewe wa zamani, Irene Uwoya na mtoto wao. Buriani kocha Katauti. 

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NDIKUMAMA WA IRENE UWOYA AFARIKI DUNIA RWANDA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top