• HABARI MPYA

    Tuesday, October 17, 2017

    SIMBA KUMKOSA MBONDE MECHI NA YANGA OKTOBA 28, BOCCO NAYE NJE WIKI MOJA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kati tegemeo wa Simba, Salim Mbonde atakuwa nje kwa mwezi mmoja baada ya kuumia Jumapili katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya timu yake ya zamani, Mtibwa Sugar uliomalizika kwa sare ya 1-1. 
    Katika kipindi hicho, Mbonde atakosa mechi nne za Ligi Kuu, kuanzia wa Jumamosi dhidi ya Njombe Mji, dhidi ya mahasimu Yanga Oktoba 28 na mbili za wiki mbili za mwanzo wa mwezi Novemba dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons. 
    Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Hajji Manara amesema leo katika mkutano na Waandishi wa Habari mjini Dar es Salaam kwamba pamoja na Mbonde, mshambuliaji John Bocco aliyeumia Jumapili pia yeye atapumzika kwa wiki moja tu. 
    Salim Mbonde atakuwa nje kwa mwezi mmoja baada ya kuumia Jumapili katika mchezo dhidi ya Mtibwa Sugar  

    “John Bocco amekwishafanyiwa vipimo na daktari ameshauri apumzike kwa wiki moja, maana yake hataweza kushiriki mchezo dhidi ya Njombe FC wakati Mbonde majeraha makubwa aliyoyapata kwenye goti yana mpelekea sasa kukaa nje na kukosa mechi nne mfululizo dhidi ya Njombe FC, Yanga, Mbeya City pamoja na Tanzania Prisons,”amesema. 
    Majeruhi wengine Simba ni kipa Said Mohammed ‘Nduda’, ambaye amepewa mapumziko ya miezi miwili baada ya kufanyiwa upasuaji nchini India wiki iliyopita na beki Shomary Kapombe ambaye matatizo yake ni makubwa na ataendelea kuwa chini ya uangalizi wa Daktari hadi atakapopona kabisa. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA KUMKOSA MBONDE MECHI NA YANGA OKTOBA 28, BOCCO NAYE NJE WIKI MOJA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top