• HABARI MPYA

    Saturday, October 21, 2017

    MTIBWA SUGAR BEGA KWA BEGA NA ‘MNYAMA’ MBIO ZA UBINGWA LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    MTIBWA Sugar imeendelea kukimbia kwa kasi ya vigogo, Simba SC baada ya leo kuibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons Uwanja wa Manungu, Turiani, mkoani Morogoro katika mfululizo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Shukrani kwake, beki Dickson Daudi Mbeikya aliyefunga bao hilo pekee la ushindi dakika ya 83 akimalizia pasi ya mkongwe mwenzake, mshambuliaji Hussein Javu.
    Kwa ushindi huo, Mtibwa Sugar inafikisha pointi 15, sawa na Simba SC ambayo sasa inaongoza Ligi Kuu kwa wastani wa mabao tu.
    Simba SC imeendeleza wimbi la ushindi katika Ligi Kuu baada ya leo kuibamiza mabao 4-0 Njombe Mji FC Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam, kiungo Muzamil Yassin akifunga mawili, Mganda Emmanuel Okwi moja sawa na Mrundi, Laudit Mavugo.
    Azam FC imetoa sare ya pili mfululizo Kanda ya Ziwa, baada ya kumaliza dakika 90 bila kufungana na Mbao FC Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, wakitoka kutoa sare ya 1-1 na Mwadui FC wiki iliyopita Shinyanga.
    Mbeya City nayo imeichapa mabao 2-0 Ruvu Shooting Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, wafungaji Elius Ambokile dakika ya 36 na Frank Hamisi Ikobelo dakika ya 52, wakati Lipuli imeichapa 1-0 Maji Maji ya Songea Uwanja wa Samora mjini Iringa, mfungaji Moka Shaaban na Ndanda FC imelazimishwa sare ya 0-0 Singida United Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.
    Kikosi cha Mtibwa Sugar leo kilikuwa; Benedictor Tinocco, Rodgers Gabriel, Issa Rashid, Cassian Ponera, Dickson Daudi, Shaaban Nditi, Ally Makarani/Hassan Dilunga, Mohammed Issa, Kelvin Sabato, Stahmil Mbonde/Hussein Javu na Salum Kihimbwa/Ismail Aidan.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR BEGA KWA BEGA NA ‘MNYAMA’ MBIO ZA UBINGWA LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top