• HABARI MPYA

    Friday, October 20, 2017

    KAGERA SUGAR CHUPUCHUPU KWA MWADUI, YACHOMOA DAKIKA ZA MWISHONI SARE 1-1

    Na Mwandishi Wetu, MWADUI
    BAO la dakika za mwishoni la Jaffary Salum Kibaya jioni ya leo limeinusuru Kagera Sugar kupoteza mechi, baada ya kupata sare ya kufungana 1-1 na wenyeji Mwadui FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Mwadui Complex, Shinyanga. 
    Kibaya alifunga bao hilo dakika ya 87 baada ya kutumia vizuri makosa ya beki wa Mwadui, David Luhende na kuisaidia Kagera Sugar ya kocha Mecky Mexime kupata ahueni.
    Mshambuliaji wa zamani wa Mbeya City na Yanga SC, Paul Nonga alianza kuifungia Mwadui FC dakika ya 10 akimchambua kipa mkongwe, Juma Kaseja kwa kichwa baada ya krosi ya Malika Ndeule.
    Kipa mkongwe Juma Kaseja leo amefungwa bao moja Kagera Sugar ikitoa sare ya 1-1 na Mwadui

    Mchezo ukawa wa timu zote kushambuliana kwa zamu, Mwadui wakitafuta mabao zaidi na Kagera Sugar kusaka la kusawazisha.
    Hata hivyo, Kagera Sugar walilazimika kusubiri hadi dakika za mwishoni kujichomoa kwenye ‘mbavu’ za Mwadui.
    Kwa matokeo hayo, Mwadui inafikisha pointi sita baada ya kucheza mechi sita na Kagera Sugar inafikisha pointi tatu baada ya kucheza mechi tatu na kuendelea kushika mmkia kwenye msimamo wa Ligi Kuu.
    Kikosi cha Mwadui FC kilikuwa; Anord Massawe, Malika Ndeule, David Luhende, Joram Mgeveke, Iddi Mobby, Awadh Juma, Morris Kaniki, Abdallah Seseme, Evarist Benard, Paul Nonga na Hassan Kabunda.
    Kagera Sugar; Juma Kaseja, Mwahita Gereza, Adeyoum Ahmed, Juma Shemvuni, Juma Nyosso, Ally Nassor, Selemani Mangoma, Ally Ramadhani, Jaffar Kibaya, Peter Mwalyanzi na Venende Ludovic.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KAGERA SUGAR CHUPUCHUPU KWA MWADUI, YACHOMOA DAKIKA ZA MWISHONI SARE 1-1 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top