• HABARI MPYA

    Monday, September 11, 2017

    WAZIRI JUNIOR APONA, AANZA KUJIFUA AZAM BAADA YA KUWAKOSA SIMBA

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI mpya wa Azam FC, Waziri Junior Shentembo kesho anatarajiwa kuanza mazoezi baada ya kupona jeraha lake la mguu wa kulia.
    Mchezaji huyo aliyesajiliwa kutoka Toto Africans ya Mwanza iliyoteremka Daraja, alikosekana katika mchezo uliopita wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Simba SC Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam Jumamosi kutokana na jeraha hilo.
    Waziri alidondokewa na chupa ya soda Alhamisi iliyomchana mguuni kiasi cha kuondolewa kwenye programu ya mechi dhidi ya Simba SC iliyomalizika kwa sare ya 0-0, lakini akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online leo mjini Dar es Salaam leo, Waziri amesema amepona na kesho ataanza mazoezi.  
    Waziri Junior Shentembo (kulia) kesho anatarajiwa kuanza 
    mazoezi baada ya kupona jeraha lake la mguu wa kulia

    “Ninamshukuru Mungu nimepona jeraha langu la mguuni na kesho kunako majaaliwa nitaanza rasmi mazoezi,”amesema Waziri mwenye kiu kubwa ya kuiona klabu yake inatwaa ubingwa wa Tanzania Bara msimu huu wa 2017/18.
    Aidha, Waziri amesifu kiwango na uwezo wa kikosi cha Azam FC katika mechi dhidi ya Simba, ingawa ilimalizika kwa sare ya 0-0. “Timu ilicheza vizuri sana Jumamosi, niseme tu hatukuwa na bahati ya kupata bao, lakini tulicheza vizuri,”amesema.
    Junior amesema kwamba baada ya kupona jeraha lake hawezi kusubiri kuingia uwanjani kuisaidia timu yake kubeba pointi zote tatu katika mchezo ujao wa Ligi Kuu dhidi ya Kagera Sugar Septemba 15, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi.
    “Ninaomba Mungu niendelee vizuri nipone, niwe fiti niweze kuichezea timu yangu katika mchezo ujao dhidi ya Kagera Sugar,”amesema Waziri.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAZIRI JUNIOR APONA, AANZA KUJIFUA AZAM BAADA YA KUWAKOSA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top