• HABARI MPYA

    Wednesday, September 06, 2017

    MGOYI MWENYEKITI KAMATI YA TUZO LIGI KUU...SANGA APETA BODI YA LIGI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeunda Kamati ya Tuzo za Wachezaji Bora wa Mwezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, chini ya Mwenyekiti, Ahmed Iddi Mgoyi, maarufu kama Msafiri Mgoyi.
    Katika Kamati hiyo, Makamu Mwenyekiti atakuwa Almasi Kasongo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Soka Dar es Salaam, wakati Katibu Mkuu ni Amir Mhando, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA).
    Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas, Kamati ya Tuzo za Ligi Kuu itakuwa inachagua wachezaji bora wa mwezi, bao bora, mwamuzi bora, kocha, kipa bora na mchezaji bora wa msimu. 
    Ahmed Iddi Mgoyi maarufu kama Msafiri Mgoyi ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Tuzo za Wachezaji Bora wa Ligi Kuu

    Wajumbe wa Kamati hiyo ni Katibu Mkuu wa zamani wa Simba SC, Patrick Kahemele, Kocha wa zamani wa Yanga, Kenny Mwaisabula, mchezani wa zamani wa kimataifa nchini, Said George na Waandishi wa Habari Ibrahim Masoud, Fatma Likwata, Salehe Ally, Gift Macha na Zena Chande.
    Wakati huo huo: Kamati ya Uchaguzi ya TFF imewapitisha Kaimu Mwenyekiti wa Yanga, Clement Sanga na Mwenyekiti wa Kagera Sugar, Hamad Yahya kuwania Uenyekiti wa Bodi ya Ligi.
    Kwa mujibu wa taarifa ya Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Revocatus Kuuli, katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti amepitishwa Shani Christoms tu, ambaye ni Mwenyekiti wa Azam FC. 
    Katika nafasi tatu za Wajumbe wa Ligi Kuu yamepitishwa majina mawili tu, Hamisi Mshuda Madaki na Ramadhani Marco Mahano, wakati kwenye nafasi mbili za Wajumbe wa Daraja la Kwanza, amepitishwa Almasi Kasongo pekee huku Brown Ernest na James Bwire wakienguliwa kwa sababu mbalimbali na Edgar Chibura amepitishwa kwenye nafasi moja ya Mjumbe wa Daraja la Pili.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MGOYI MWENYEKITI KAMATI YA TUZO LIGI KUU...SANGA APETA BODI YA LIGI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top