• HABARI MPYA

    Thursday, September 21, 2017

    MBAO FC YAITULIZA SIMBA KIRUMBA, SARE 2-2

    Na Rehema Lucas, MWANZA
    KWA mara ya kwanza, Mbao FC leo imefanikiwa kutopoteza mechi dhidi ya Simba SC baada ya kulazimisha sare ya 2-2 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara uliofanyika Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
    Sare hiyo ya pili kwa Simba ndani ya mechi nne – inamaanisha Wekundu wa Msimbazi bado hawajapata dawa ya kushinda mechi za ugenini, kufuatia awali kulazimishwa sare ya 0-0 na Azam FC Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Mechi nyingine, Simba imeshinda 7-0 dhidi ya Ruvu Shooting na 3-0 dhidi ya Mwadui FC zote Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.   
    Shiza Kichuya (kushoto) baada ya kufunga bao la kwanza la Simba leo katika sare ya 2-2 na Mbao FC 





    Katika mchezo wa leo uliochezeshwa na refa Athumani Lazi wa Morogoro, hadi mapumziko Simba walikuwa mbele kwa bao 1-0, lililofungwa na winga machachari, Shiza Ramadhani Kichuya dakika ya 16 akimalizia krosi nzuri ya beki Erasto Edward Nyoni.
    Kichuya alishindwa kuendelea na mchezo dakika ya 44 baada ya kuumia na kumpisha Haruna Niyozima, wakati Mbao nalo walimtoa Said Said dakika ya 37 na kumuingza Herbet Lukindo.
    Kipindi cha pili Mbao walirudi kwa kasi nzuri na kufanikiwa kusawazisha bao dakika ya 46 tu, kupitia kw3a Habib Kiyombo ambaye hilo linakuwa bao lake la tatu msimu huu.
    Hata hivyo, Simba walijibu kwa mashambulizi mfululizo na kufanikiwa kupata bao la pili dakika tatu baadaye, mfungaji kiungo Mghana, James Kotei.   
    Mbao hawakukata tamaa, waliendelea kushambulia na kufanikiwa kusawazisha tena dakika ya 81 kupitia Emmanuel Mvuyekire aliyefunga kwa shuti la mbali pia.
    Kutoka hapo timu zote ziliendelea kushambuliana kwa zamu, lakini hakukuwa na mabao zaidi.
    Ikumbukwe msimu uliopita, Simba ilishinda mechi zote tatu ilizokutana na Mbao, zikiwemo mbili za Ligi Kuu msimu uliopita Alhamisi ya Oktoba 20 iliposhinda 1-0 Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na Jumatatu ya Aprili 10 iliposhindaa 3-2 Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
    Mchezo mwingine ulikuwa wa fainali ya Kombe la Azam Sports Federation Cup Mei 27, mwaka huu ambao Simba walishinda 2-1 ndani ya dakika 120 Uwanja wa Jamhuri Dodoma.
    Kikosi cha Mbao FC kilikuwa; Kelvin Ingendelezi, Boniphace Maganga, Abubakar Ngalema, Yusuph Mgeta, Yusuph Ndikumana, Sadallah Lipangile, Ibrahim Njohole/Emmanuel Mvuyekire, Hussein Kassanga, Moses Shaaban, Said Said/Herbet Lukindo dk37 na Habibu Kiyombo/Ndaki Kisambale dk62.
    Simba: Aishi Manula, Erasto Nyoni, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Juuko Murshid, Method Mwanjali, James Kotei, Nicholaus Gyan/Juma Luizio dk76, Muzamil Yassin, John Bocco, Emmanuel Okwi na Shiza Kichuya/Haruna Niyonzima dk44. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBAO FC YAITULIZA SIMBA KIRUMBA, SARE 2-2 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top