• HABARI MPYA

    Monday, August 14, 2017

    TSHITSHIMBI ASAINI MIAKA MIWILI YANGA, KESHO ANAKWENDA PEMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    HATIMAYE kiungo Papy Kabamba Tshishimbi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), leo amesaini mkataba wa miaka miwili kujiunga na mabingwa wa Tanzania, Yanga SC.
    Mchezaji huyo alikuwa nchini wiki iliyopita kwa ajili ya vipimo vya afya na baada ya kufaulu akaambiwa afuate barua ya kuruhusiwa na klabu yake, Mbabane Swallows ya Swaziland kuondoka ili aje kusaini mkataba.
    Baada ya kukamilisha taratibu hizo, Tshishimbi leo amesaini mkataba wa miaka miwili mbele ya Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Hussein Nyika mabao ya klabu, Jangwani, Dar es Salaam. 
    Papy Kabamba Tshitshimbi akikandamiza dole gumba kwenye fomu za Yanga leo Dar es Salaam
    Na baada ya kusaini mkataba huo, mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 ambaye inaaminika ndiye mrithi wa Mnyarwanda, Haruna Niyonzima aliyekwenda kwa mahasimu Simba, anatarajiwa kuondoka kesho Dar es Salaam kwenda kisiwani Pemba kuungana na kikosi cha Yanga kwa maandalizi ya mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya mahasimu wa jadi, Simba Agosti 23.
    Yanga ilivutiwa na Tshishimbi baada ya kumuona akiichezea Swallows katika mchezo wa Kombe la Shirikisho la Soka Afrika mapema mwaka huu Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
    Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa (kushoto) akimshuhudia Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu, Hussein Nyika akisaini mkataba na Papy Kabamba Tshitshimbi leo 
    Baada ya hapo ikamfuatilia kwenye mchezo wa marudiano Swaziland ambao aliingoza Mbabane Swallows kuichapa Azam 3-0 na kusonga mbele. Tangu hapo, Yanga imekuwa na mawasiliano na mchezaji huyo kwa lengo la kumsajili, ndoto ambazo zimetimia.    
    Tshitshimbi anakuwa mchezaji wa sita wa kigeni wa Yanga kati ya saba wanaotakiwa kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya kipa Mcameroon, Youthe Rostand, Wazimbabwe, kiungo Thabani Kamusoko na mshambuliaji Donald Ngoma na washambuliaji Mrundi Amissi Tambwe na Mzambia Obrey Chirwa.
    Yanga inataka kuziba nafasi ya saba kwa kusajili beki wa kati kuziba pengo la Mtogo, Vincent Bossou aliyeondoka pia baada ya kumaliza mkataba kufuatia kuitumikia klabu huyo kwa misimu miwili. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TSHITSHIMBI ASAINI MIAKA MIWILI YANGA, KESHO ANAKWENDA PEMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top