• HABARI MPYA

    Saturday, August 19, 2017

    MAVUGO APIGA MBILI, SIMBA YAITANDIKA 5-0 GULIONI FC

    Na Mwandishi Wetu, ZANZIBAR
    SIMBA SC imeibuka na ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Gulioni FC katika mchezo wa kirafiki usiku huu Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Katika mchezo huo maalum wa kujiandaa na mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya mahasimu, Yanga Jumatano Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam – Simba waliizidi kila idara Gulioni inayocheza Daraja la Kwanza visiwani Zanzibar.
    Mshambuliaji Mrundi, Laudit Mavugo alikuwa kwenye kiwango kizuri leo na amefunga mabao mawili dakika za 13 na 40, wakati mabao mengine yamefungwa na wachezaji wa zamani wa Mtibwa Sugar, Shiza Kichuya dakika ya 37, Juma Luizio dakika ya 41 na Mohammed Ibrahim ‘Mo’ dakika ya 67.
    Laudit Mavugo amefunga mabao mawili Simba ikishinda 5-0 leo dhidi ya Gulioni FC 

    Huo ni mchezo wa pili kwa Simba katika kambi yake ya Unguja kujiandaa na mchezo dhidi ya Yanga, baada ya Alhamisi kulazimishwa sare ya 0-0 na Mlandege ya Ligi Kuu Zanzibar.
    Watani wao wa jadi, Yanga wapo Pemba pia kwa maandalizi ya mchezo huo na kesho nao watacheza mechi ya pili visiwani humo, watakapomenyana na Jamhuri Uwanja wa Gombani, Pemba baada ya Jumapili ya wiki iliyopita kushinda 2-0 dhidi ya Mlandege Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
    Kikosi cha Gulioni FC kilikuwa; Haji Yussuf, Ibrahim Hamisi, Shaaban Hassan, Mohammed Omar, Nuhu Ally, Ulele Uledi, Hamad Kawamba, Ally Mbaraka, Ally Amour, Ally J Kipanga na Fahim Khalfan.
    Simba SC; Aishi Manula/EmManuel Mseja, Erasto Nyoni, Ally Shomary/Mohammed Hussein ‘Thshabalala’, Salim Mbonde, Method Mwanjali/Paul Bundala, James Kotei/Jonas Mkude, Haruna Niyonzima/Mwinyi Kazimoto, Muzamil Yassin/Said Ndemla, Laudit Mavugo/Mohammed ‘Mo’ Ibrahim, Juma Luizio na Shiza Kichuya/Jamal Mnyate. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAVUGO APIGA MBILI, SIMBA YAITANDIKA 5-0 GULIONI FC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top