• HABARI MPYA

    Saturday, August 19, 2017

    LIBYA, MOROCCO ZA KWANZA KUFUZU CHAN, MISRI NA ALGERIA NJE

    LIBYA imekuwa timu ya kwanza kufuzu Michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) mwakani nchini Kenya baada ya sare ya 1-1 na Algeria mjini Sfax, ikiungana na Morocco iliyoitandika Misri 3-1 mjini Rabat jana.
    Washindi hao wa mwaka 2014 nchini Afrika Kusini, Libya wanafunzu kwa ushindi wa jumla wa  3-1 baada ya ushindi wa 2-1 kwenye mchezo wa kwanza mjini Constantine wiki iliyopita.
    Hii inakuwa mara ya tatu kwa kufuzu kwenye fainali hizo zilizofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 2009 zikiwa zinakutanisha wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee.
    Licha ya kuupeleka mchezo huo katika wa Sfax nchini Tunisia kutokana na machafuko ya kisiasa nchini mwao, bado Libya ilitawala mchezo huo ikibebwa na wachezaji wengi wa Ahly Tripoli iliyofuzu Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Algeria ambao walishika nafasi ya nne katika CHAN pekee waliyoshiriki mwaka 2011 nchini Sudan walikuwa wa kwanza kupata bao dakika ya 23 kupitia kwa kiungo wa MC Alger, Sofiane Bendebeka aliyemchamua kipa wa Libya, Mohamed Nashnush.
    Nyota kinda wa Ahly Tripoli, Muaid Ellafi, aliyefunga bao la ushindi kwenye mechi ya kwanza na jana pia aliwaumiza Walgeria baada ya kufunga bao la kusawazisha dakika ya 45.
    Katika mchezo mwingine mjini Rabat, wenyeji Morocco walimalizia kazi vizuri na kuitoa Misri kwa kuichapa 3-1 mabao ya beki Jawad El Yamiq dakika ya 50 akimalizia mpira wa adhabu wa Abdelilah Hafidi, Abderrahim Makran dakika ya 53 na Badr Boulhroude kwa penalti dakika ya 69 na Misri wakapata bao la kufutia machozi baada ya Hamza Semmoumy kujifunga dakika 85.
    Morocco wanafuzu kwa ushindi wa jumla wa 4-2 hizo zikiwa fainali zao za tatu za CHAN baada hya mwaak 2014 na 2016 Afrika Kusini na Rwanda. Timu nyingine 12 za kukamilisha washiriki wa CHAN ya Kenya zitapatikana wikiendi hii, yaani leo na kesho.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LIBYA, MOROCCO ZA KWANZA KUFUZU CHAN, MISRI NA ALGERIA NJE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top