• HABARI MPYA

    Thursday, August 17, 2017

    GYAN WA SIMBA AOMBA KUCHEZEA TAIFA STARS BAADA YA KUTEMWA BLACK STARS B

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa zamani wa Ebusua Dwarfs, Nicholas Gyan ameonyesha dhamira ya kuukana uraia wa nchi yake, Ghana na kuchukua wa Tanzania.
    Gyan amejiunga na Simba SC ya Dar es Salaam mapema mwezi huu kwa mkataba wa miaka mitatu kutoka Ebususa ya ligi ya kwao, lakini kitendo cha kuondolewa kwenye timu ya taifa ya Ghana ya wachezaji wa nyumbani, maarufu kama Black Stars B kimemkera na sasa anataka kuhamia Tanzania moja kwa moja.
    “Nimekataliwa na kutoswa na watu wangu mwenyewe na sitajali kuchezea nchi nyingine yoyote itakayoniomba. Nawezaje kukosekana kwenye Black Stars B baada ya kufunga mabao 11 kwenye msimu?” alisema Gyan akizungumza na kipindi cha Final Whistle Talkshow cha kwao, Ghana.
    Nicholas Gyan ameonyesha dhamira ya kuukana uraia wa nchi yake, Ghana na kuchukua wa Tanzania

    Gyan alikuwemo kwenye kikosi cha Black Stars B kilichokuwa kinajiandaa na mechi ya kufuzu Fainali za Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) mwaka 2018 dhidi ya Burkina Faso kabla ya kwenda Tanzania kutambulishwa katika klabu yake mpya, Simba.
    Na baada ya kuichezea katika mechi ya kwanza Simba SC ikiifunga klabu bingwa ya Rwanda 1-0, Rayon Sport katika tamasha la Simba Day – Gyan alirejea Ghana kutafuta nafasi ya kutimiza ndoto zake za kuichezea Black Stars B mechi dhidi ya Burkina Faso.
    Hata hivyo, mchezaji huyo aliyefunga mabao 11 katika Ligi Kuu ya Ghana inayoendelea akakuta ameondolewa kabisa kwenye kikosi kwa sababu amesaini nje ya nchi na michuano ya CHAN ni kwa ajili ya wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee.
    Japokuwa Gyan amekasirika na anataka kuwa raia wa Tanzania, lakini alichofanyiwa nchini mwake ni sahihi kwa mujibu wa sheria za Shirikisho la Soka Afrika (CAF) – baada ya kusaini tu mkataba na klabu ya nyingine maana yake amejiondoa kwenye orodha ya wachezaji wanaocheza Ghana.
    Kwa Tanzania itakuwa neema kumpata mchezaji mwenye kipaji kama Gyan Taifa Stars, hususan mshambuliaji na kijana mdogo kama yeye ambaye Desemba 23, mwaka huu atafikisha umri wa miaka 20.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: GYAN WA SIMBA AOMBA KUCHEZEA TAIFA STARS BAADA YA KUTEMWA BLACK STARS B Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top