• HABARI MPYA

    Wednesday, July 05, 2017

    MGOMBEA URAIS TFF AMTOLEA UVIVU KARIA, ASEMA AMEKIUKA...

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MGOMBEA Urais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Shijja Richard amepinga kitendo cha mgombea mwenzake, Wallace Karia kuingikia mchakato wa uchaguzi uliopangwa Agosti 12, mwaka huu Dodoma isivyo stahili.
    "Nimesikitishwa na kitendo cha mgombea mwenzangu urais wa TFF, Wallace Karia kushiriki mchakato wa uchaguzi kwa kuongoza kikao cha Kamati ya Utendaji kilichoteua wajumbe wa Kamati ya Uchaguzi huku akijua yeye ni mgombea tena wa nafasi nyeti ya urais,".
    Kauli ya Shijja, Ofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Mwandishi wa Habari wa zamani wa gazeti la Majira, inafiatia Kamati ya Utendaji ya TFF jana kuvunja Kamati ya Uchaguzi na kuteua Kamati nyingine kusimamia uchaguzi huo.
    Ofisa wa TRA, Shijja Richard ambaye pia Mwandishi wa Habari wa zamani amempinga Kaimu Rais wa TFF, Wallace Karia kuingilia mchakato wa uchaguzi isivyo kawaida

    Katika taarifa yake kwa vyombo vya Habari, Shijja amesema uamuzi huo ulitokana na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Wakili Msomi Revocatus Kuuli kutumia mamlaka yake kisheria na kuamua kusimamisha mchakato wa uchaguzi baada ya kutokea kutokuelewana ndani ya Kamati hiyo.
    Amesema kwa mujibu wa maelezo ya Wakili Msomi Kuuli aliyoyatoa baada ya kutokea kutokuelewana huko wajumbe walitofautiana kwa kutaka kuwakata wagombea bila sababu za msingi na kutaka Rais wa TFF Jamal Malinzi apitishwe bila kufanyiwa usaili.
    Kutokana na utata huo, Kamati ya Utendaji ya TFF iliamua kuwafuta wajumbe wa Kamati mbalimbali ikiwemo Kamati ya uchaguzi na kumuacha mwenyekiti wake Wakili Msomi Kuuli.
    Wajumbe walioenguliwa kwenye Kamati ya uchaguzi ni Wakili Msomi Domina Madeli aliyekuwa Makamu Mwenyekiti, Juma Lalika, Jeremiah Wambura na Omary Hamidu.
    Wajumbe wapya walioteuliwa kuungana na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi Wakili Msomi Kuuli ni Wakili Msomi Mh Mohammed Mchengela (MB), Wakili Msomi Malangwe Ally, Wakili Msomi Kilomoni Kabamba na Wakili Msomi Deus Kalua.
    "Karia ana mgongano wa maslahi katika suala zima la uchaguzi kwa sababu naye ni mgombea wa nafasi nyeti ya urais. Katikati ya mchakato wa uchaguzi anaposhiriki kuongoza kikao kinachoteua Kamati ya Uchaguzi ni suala ambalo linaashiria kutokuwepo kwa haki katika mchakato mzima,".
    "Msimamo wa kisheria unahitaji siyo tu kwamba haki itendeke, bali pia ionekane imetendeka. Kama mtakumbuka Karia aliwekewa pingamizi la uraia wake na mmoja ya wagombea wa urais. Anaposhiriki kama kiongozi mkuu kufuta Kamati iliyokuwa inajadili pingamizi juu ya uraia wake na kuunda nyingine inatoa picha ya kuwapo nguvu ya ziada katika kusukuma mchakato wa uchaguzi uende kwa upendeleo,"amesema Shijja.
    Katika mazingira kama haya hata kama haki itatendeka, haiwezi kuonekana kama imetendeka. Hii ni dosari kubwa sana kwenye huu uchaguzi. Nafahamu kwamba Kamati ya Utendaji imetumia mamlaka yake kikatiba kufuta na kuunda Kamati mpya ya Uchaguzi pamoja na Kamati nyingine,"amesema.
    Shijja amesema lakini wajumbe wengi wa Kamati ya utendaji ni wagombea, wameenda kuteua Kamati itakayoshiriki kuwachuja, hivyo ameuita  ubabaishaji mwingine ndani ya mpira wa miguu Tanzania.
    Amesema busara ya kawaida ilikuwa inahitaji kutumika, Kaimu Rais Karia akiri mgongano wa maslahi (declaration of conflict of interest) na kujitoa katika mchakato huo.
    "Nawaomba ndugu zangu kama tunataka kuleta mabadiliko ya kweli katika kuendesha mpira wa miguu inabidi tusikubali ubabaishaji wa aina hii katika mpira. Bila hivyo tunaendelea kuwa kichwa cha mwendawazimu kila kukicha kwa sababu watendaji wetu wanafanya hila kutekeleza matakwa yao kuanzia kwenye Uchaguzi,"amesema.
    "Mtu ambaye anasimamia figisu katika mchakato wa uchaguzi ama kwa rushwa au kwa njia nyingine yoyote tusitarajie uongozi bora kutoka kwake.
    Kamati ya Uchaguzi ingetengenezwa kwa mazingira huru, ingeachwa ifanye kazi yake kwa uhuru na wajumbe wangeachwa wafanye maamuzi yao kwa uhuru bila vishawishi vya rushwa wala upendeleo hapo tungeweza kupata viongoZi bora katika kuendesha mpira wa miguu.
    Shijja ameonya vyanzo vya matatizo ya uongozi katika mpira huwa vinaanzia kwenye uchaguzi. Tuache ubabaishaji. Tutengeneze mchakato wa haki ili kupata viongoZi bora watakaoweza kusimamia mabadiliko makubwa katika uendeshaji wa mpira wetu.
    Akijibu madai hayo ya Shijja, Karia ametaka mgombea mwenzake huyo kufuata taratibu kama anaona kuna jambo limekiukwa. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MGOMBEA URAIS TFF AMTOLEA UVIVU KARIA, ASEMA AMEKIUKA... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top