• HABARI MPYA

    Wednesday, June 07, 2017

    TSHABALALA KUWAKOSA MAMBA JUMAMOSI TAIFA

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kushoto wa kimataifa wa Tanzania, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ ataukosa mchezo wa kwanza wa Kundi L kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2019 nchini Cameroon dhidi ya Lesotho Jumamosi.
    Taifa Stars watakuwa wenyeji wa Mamba Jumamosi kuanzia Saa 2:00 usiku Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, lakini kocha wa Tanzania, Salum Mayanga amesema atamkosa Tshabalala kwa sababu ni majeruhi.   
    Mayanga amesema kwamba Tshabalala hayuko fiti kwa mchezo huo na pamoja na jitihada za madaktari kumponya, lakini atakosekana Jumamosi.
    Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ ataukosa mchezo dhidi ya Lesotho Jumamosi kutokana na kuwa majeruhi

    Tshabalala hakumaliza mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), au Azam Sports Federation Cup (ASFC) Simba ikiifunga Mbao 2-1 Mei 27, mwaka huu Uwanja wa Jamhuri, Dodoma baada ya kutolewa kipindi cha kwanza tu kufuatia kuumia.
    Na tangu siku hiyo, pamoja na matibabu mazuri ambayo amekuwa akipatiwa, lakini beki huyo aliyeibuliwa kwenye akademi ya Azam FC kabla ya kwenda kuanza kupata uzoefu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara timu ya Kagera Sugar ya Bukoba iliyomfanya aonekane Simba SC hajacheza mpira.
    Taifa Stars imerejea leo kutoka mjini Alexandria, Misri ambako ilikuwa imeweka kambi ya wiki moja kujiandaa na mchezo dhidi ya Lesotho. 
    Na baada ya kuwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam mchana wa leo, Mayanga amesema; “Tunamshukuru Mungu tumerudi salama na kambi ilikuwa nzuri, kitu ambacho kilitupa wepesi sisi kufanya mazoezi vizuri. Tumerudi nyumbani na tutaendelea na mazoezi leo usiku kama kawaida,”.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TSHABALALA KUWAKOSA MAMBA JUMAMOSI TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top