• HABARI MPYA

    Wednesday, June 07, 2017

    SAKHO AFURAHIA ZIARA YAKE TANZANIA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kimataifa wa Ufaransa, Mamadou Sakho anayechezea Liverpool ya England akiwa na mkewe, Majda na mabinti zao wawili wamefurahia ziara yao kitalii nchini.
    Mchezaji huyo ambaye msimu uliopita alicheza kwa mkopo Crystal Palace amepsoti video fupi kwenye ukurasa wake wa Instagram akisema; “Karibuni safari Tanzania” na mkewe na mabinti zake wakadakia kwa furaha; “Jambo jambo”.
    Na baada ya hapo wafanyakazi wa mbuga ya wanyama waliyotembelea wakawaimbia wimbo mzuri wa Jambo, huku wakipiga makofi.
    Hakika lilikuwa ni tukio la kupendeza na ilionekana kama Sakho ndiyo anaondoka baada ya kuwepo kwake nchini kwa siku tatu.  
    Mamadou Sakho akiwa na mkewe, Majda (kushoto) wamewabeba mabinti zao wawili  

    Sakho alionekana kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Juni 5, ikiwa ni siku mbili tu baada ya Nahodha na kiungo wa zamani wa kimataifa wa England, David Beckham kuondoka nchini kufuatia wiki moja ya kutalii kwenye vivutio mbalimbali, ikiwemo mbuga ya wanyama ya Serengeti.
    Sakho aliyezaliwa Februari 13, mwaka 1990, kisoka aliibukia Paris FC kabla ya kuhamia timu ya vijana ya Paris Saint-Germain mwaka 2002 na Oktoba mwaka 2007 aliweka rekodi ya mchezaji kijana daima kuiongoza timu hiyo kam Nahodha katika Ligue 1. 
    Sakho amecheza mechi zaidi ya 200 katika klabu hiyo, akishinda nayo mataji yote manne ya nyumbani kabla ya mwaka 2013 kuuzwa Liverpool kwa dau la Pauni Milioni 18.
    Mwaka huu alitolewa kwa mkopo Crystal Palace pia ya Ligi Kuu England ambako amekwenda kucheza mechi nane.
    Sakho ni mchezaji wa kikosi cha kwanza cha wakubwa cha Ufaransa, ambaye awali amechezea timu zote za vijana na za nchi hiyo.
    Tangu acheze mechi yake ya kwanza kikosi cha wakubwa cha Ufaransa mwaka 2010 dhidi ya England, Sakho amecheza mechi zaidi ya 25 na alikuwemo kwenye kikosi cha timu hiyo kwenye Fainali za Kombe la Dunia  mwaka 2014 nchini Brazil.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAKHO AFURAHIA ZIARA YAKE TANZANIA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top