• HABARI MPYA

    Sunday, June 11, 2017

    MACHUPPA ASHAURI TFF ITAFUTE KOCHA MKUBWA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Athumani Machuppa ameshauri Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) litafute kocha wa kiwango cha juu kwa ajili ya timu ya taifa, Taifa Stars, kwani Salum Mayanga peke yake hawezi. 
    Ushauri huo wa mchezaji huyo wa zamani wa Simba ya nyumbani na Vasalunds IF ya Sweden, unafuatia Taifa Stars kulazimishwa sare ya 1-1 na Mamba wa Lesotho katika mchezo wa kwanza wa Kundi L kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2019 Cameroon.
    Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Azan Complex, Chamazi, Dar es Salaam, Stars ilitangulia kwa bao la Nahodha wake, Mbwana Ally Samatta dakika ya 27 kwa shuti zuri la mpira wa adhabu, kabla ya Mamba kusawazisha kupitia kwa Thapelo Tale dakika ya 34.
    Athumani Machuppa ameishauri TFF itafute kocha mkubwa wa kuiongoza Taifa Stars 

    Na mara tu baada ya mchezo, Machuppa akaposti katika ukurasa wake wa Facebook; “Kwani kuna ubabaishaji gani kutafuta kocha wa maana mwenye Cv za Kutosha....timu yetu haichezi kitimu, hatujui mashambulizi yaanzie wapi, kiongozi wetu pekee Mbwana Ally Samatta,”alisema.
    “Natamani kuona tunapata kocha mkubwa, ambaye atasaidiana na Mayanga, kikosi cha Stars cha mechi ya mwisho kilikuwa kizuri mno kiwango chao, lakini sielewi...nimebahatika kuangalia mechi kipindi kimoja cha mwisho, ila mapungufu ni mengi mno,”aliongeza.
    Machuppa aliyekuwemo kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichotwaa Kombe ka CECAFA Castle mwaka 2002 Mwanza, amesema kwamba kama Tanzania tuna mpango wa kwenda fainali za AFCON 2019 tuamke kabla jua halijakuchwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MACHUPPA ASHAURI TFF ITAFUTE KOCHA MKUBWA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top