• HABARI MPYA

    Tuesday, May 16, 2017

    SIMBA KUKAA MEZANI NA MO DEWJI LEO KUMALIZA TOFAUTI ZAO

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    UONGOZI wa Simba SC leo unatarajiwa kukutana na mfanyabiashara Mohammed ‘Mo’ Dewji katika kikao maalum cha kumaliza tofauti zilizojitokeza baada ya klabu kuingia mkataba wa udhamini na kampuni ya SportPesa. 
    Na hiyo inafuatia kikao cha suluhu juzi kuamkia jana baina ya Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe na Kamati ya Utendaji ya klabu chini ya Rais, Evans Elieza Aveva. 
    Hans Poppe alijiuzulu Ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba juzi na maana yake kujivua pia na uongozi wa Kamati ya Usajili na ya ujenzi wa Bunju Complex baada ya kuchukizwa na kutohusishwa katika mkataba wa udhamini wa kampuni ya SportPesa.
    Rais wa Simba, Evans Aveva (kushoto) akiwa na Mohammed Dewji (kulia)
    “Siyo kushirikishwa mimi tu, bali Wajumbe wengine wa Kamati ya Utendaji pia, lakini kubwa zaidi tuna makubaliano na Mo (Dewji) kuwa tukitaka kuingia mkataba na yeyote yule, hakatai lakini tumshirikishe, sasa tunasaini mkataba kwa kumzunguka ni kukosa uungwana na siwezi kuwa sehemu ya hilo,”alisema akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online juu ya kujiuzulu kwake.
    Poppe alisema kwamba alijaribu sana kutaka kukutana na viongozi wa Simba kujadili nao suala hilo, lakini walikuwa wanamkwepa ndiyo maana akaamua kujiuzulu; “Hatujakaa, kila nikiwaambia tulijadili wanaingilia huku wanatokea kule,” alisema juzi usiku.
    Lakini jana Poppe alisema kufuatia kikao chake na uongozi wa Simba juzi usiku wamemaliza tofuti hizo na kufikia makubaliano ya kurudi kuzungumza na Mo Dewji wamalize utata uliopo. 
    Dewji anayetaka kununua hisa Simba, alikasirishwa na uongozi wa klabu hiyo kwa kuingia mkataba wa udhamini na kampuni ya SportPesa bila kumshirikisha.na akataka alipwe fedha zake, Sh Bilioni 1.4 alizokuwa anaikopesha Simba kwa kulipa mishahara ya wachezaji na benchi la Ufundi, Sh Milioni 80 kila mwezi.
    Ikumbukwe Mo alikubaliana na uongozi wa Simba kununua asilimia 51 ya hisa kwa Sh. Bilioni 20 mara baada ya mchakato wa mabadiliko ya Katiba utakapokamilika. Na katika makubaliano ya msingi baina yake na uongozi ni kwamba ikitokea kampuni inataka kuidhamini klabu ashirikishwe, jambo ambalo halikufanyika.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA KUKAA MEZANI NA MO DEWJI LEO KUMALIZA TOFAUTI ZAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top