• HABARI MPYA

    Tuesday, May 16, 2017

    KUNDI B LADHIHIRISHA KWELI NI LA KIFO AFCON U-17 AFRIKA

    Na Mahmoud Zubeiry, LIBREVILLE
    MICHEZO yote ya Kundi B Fainali za Mataifa ya Afrika Vijana chini ya umri wa miaka 17 kuanza kwa sare jana Uwanja wa l’Amitie Sino mjini Libreville, Gabon inamaanisha kundi hilo ni gumu.
    Mabingwa watetezi, Mali walimiliki mpira kwa muda mrefu jana, lakini wakashindwa kuifunga Tanzania inayocheza mashindano ya ngazi hii kwa mara ya kwanza na mwishowe wakatoka sare ya 0-0.
    Na baadaye Angola na Niger zikakutana katika mchezo mwingine mkali zaidi na wa kusisimua na kufungana mabao 2-2.
    Wachezaji wa Tanzania wakiwasalimia wachezaji wa Mali kabla ya mchezo wa jana

    Hii ni tofauti sana na mechi za Kundi A juzi, ambazo ‘mvua ya mabao’ ilishuhudiwa ikimiminika Uwanja wa Port Gentil.
    Kwanza wenyeji Gabon walifungwa mabao 5-1 na Guinea kabla ya mabingwa mara mbili, Ghana kuitandika 4-0 Cameroon.
    Leo ni mapumziko na michuano hiyo inatarajiwa kuendelea kesho kwa mechi za Kundi A, Guinea wakimenyana na Cameroon na Ghana wakipepetana na Gabon Uwanja wa Port Gentil.
    Mechi za Kundi B zitarudi Alhamisi ya Mei 18, Tanzania wakianza na Angola kabla ya Mali kupepetana na Niger Uwanja wa l’Amitie Sino mjini Libreville.
    Hatua ya makundi inatarajiwa kuhitimishwa Mei 20 na 21 mwaka huu, Kundi A Gabon wakimaliza na Cameroon na Guinea na Ghana Uwanja wa Port Gentil kabla ya siku inayofuata, Mali kuanza na Angola na baadaye Tanzania kumalizana na Niger.
    Timu mbili za juu katika kila kundi pamoja na kwenda Nusu Fainali, pia zitajihakikishia tiketi ya kucheza Fainali za kombe la Dunia la U-17 Oktoba mwaka huu nchini India.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KUNDI B LADHIHIRISHA KWELI NI LA KIFO AFCON U-17 AFRIKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top