• HABARI MPYA

    Saturday, May 13, 2017

    AZAM YAICHIMBIA KABURI TOTO AFRICANS, YAIPIGA 2-0 CHAMAZI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    UKITAKA kumuua nyani, usimtazame usoni. Usemi huo umedhihirika leo, baada ya Azam FC kuwatandika 2-0 Toto Africans ya Mwanza ambao wapo hatarini kushuka daraja.
    Ikihitaji hisani ya ushindi ili kujiepusha na balaa la kushuka Daraja, Toto Africans ilijikuta inatota kwa mabao ya mshambuliaji chipukizi, Shaaban Iddi Chilunda kipindi cha kwanza na winga Ramadhani Singano ‘Messi’ kipindi cha pili.
    Chilunda alianza kufunga dakika ya 12 kwa kichwa akimalizia krosi safi ya Mzimbabwe, Bruce  Kangwa kabla ya Messi kufunga la pili dakika ya 50 baada ya kuwazidi maarifa mabeki wa Toto.
    Shaaban Iddi alifunga bao la kwanza leo Azam ikishinda 2-0 Uwanja wa Azam Complex
    Kwa matokeo hayo, Azam FC inafikisha pointi 52 baada ya kucheza mechi 29 na kuendelea kushika nafasi ya tatu, nyuma ya mabingwa watetezi, Yanga pointi 62 za mechi 27 na Simba SC pointi 65 za mechi 27.
    Hali ni mbaya kwa Toto, ambayo inabaki na pointi zake 29 za mechi 28 katika nafasi ya 14, moja ya nafasi tatu za mkiani za kushuka daraja, mbele ya JKT Ruvu ambayo tayari imekwishateremka na Maji Maji ya Songea yenye pointi 29 za mechi 28 pia, lakini inazidiwa wastani wa mabao.
    Kikosi cha Azam FC kilikuwa; Aishi Manula, Bruce Kangwa, Daniel Amoah, Aggrey Morris, 
    Yakubu Mohammed, Erasto Nyoni, Shomari Kapombe, Ramadhani Singano ‘Messi’/Masoud Abdallah dk86, Shaaban Iddi/Khamis Mcha ‘Vialli’ dk70 na John Bocco.
    Toto Africans; David Kisu, Juvenary Joseph/Juma Soud dk68, Ramadhani Malima/Ladislaus Mbogo dk78, Reliant Lusajo, Hamim Karim, Yussuf Mpili, Carlos Kirenge, Hussein Kasanga, Waziri Junior, William Joshua/Hamad Mbumba dk62 na Jaffar Mohammed.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM YAICHIMBIA KABURI TOTO AFRICANS, YAIPIGA 2-0 CHAMAZI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top