• HABARI MPYA

    Friday, May 12, 2017

    AZAM FC KUANDAA MASHINDANO YA VIJANA KUANZIA U-11 HADI U-17

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, inayofuraha kutangaza uzinduzi wa programu ya Ligi za Vijana za Azam (AYL), ambayo utaifanya klabu kuendesha ligi za vijana za timu chini ya umri wa miaka 11, 13, 15 na 17 ndani ya mkoa wa Dar es Salaam.
    Kwa kuanzia, Azam FC itaanza na Ligi ya Vijana ya chini ya umri wa miaka 13 itakayoanza Mei 27, mwaka huu katika Uwanja wa Azam Complex, ambapo mechi zitakuwa zikifanyika kila Jumamosi kwa muda wa wiki 10.
    Akizungumza jana mjini Dar es Salaam, Mkuu wa Maendeleo ya Soka la Vijana la Azam FC, Tom Legg, alisema kuwa wanayofuraha kufanya kazi na timu sita za hapa kwa kuanzia kwenye ligi hiyo, ambazo ni Bom Bom SC, JMK Park Academy, Rendis FC, Ilala Academy, Magnet Youth pamoja na wenyeji Azam, ambao wataumana kuwania taji la michuano hiyo (U-13).
    Mkuu wa Maendeleo ya Soka ya Vijana Azam FC, Tom Legg (kulia) akiwa katika moja ya shughuli zake  

    Legg alisema kuwa kutokana na klabu kuonyesha dhamira ya uaminifu na uwazi katika maendeleo ya soka la vijana, kila mchezaji atakayeshiriki michuano ya Ligi ya Vijana ya Azam atatakiwa kutoa ushahidi wa utambulisho kuhusu umri wakati atakapokuwa akijiandikisha kushiriki ligi hiyo.
    “Taarifa hizo zitahifadhiwa kwenye mtandao, zitashirikishwa miongoni mwa timu shiriki na zitakuwa zikipatikana kwa makocha wote kwenye simu zao za kisasa ili kuhakikisha kuwa kila mchezaji atakayecheza kwenye ligi hiyo atakuwa amesajiliwa na Kamati ya Maandalizi na kuwa na umri sahihi,” alisema.
    Mtaalamu huyo wa soka la vijana, alisema kuwa hatua ya pili ya Ligi ya Vijana ya Azam, itakuwa ni uzinduzi zile za chini ya umri wa miaka 15 na 17 utakaofanyika Agosti mwaka huu, huku akidai katika siku chache zinazokuja Azam FC itatoa taarifa za ziada kuhusu hili na kwa timu ambazo zitavutiwa kushiriki kudhibitisha ushiriki wao kwa kujisajili.
    Aidha alisema mipango ya hapo baadaye ni kuendesha ligi za aina hiyo kwenye mikoa mingine ya Tanzania na akiwa kama Mkuu wa soka hilo la vijana amedai kuwa amekuwa akifanya kazi bila kuchoka uwanjani itakayopelekea hapo baadaye klabu kuipanua zaidi programu hiyo.
    Alisema lengo kuu la kuanzishwa kwa programu ya Ligi ya Vijana ya Azam FC ni kuhakikisha klabu hiyo inacheza nafasi kubwa katika maendeleo ya kutengeneza kizazi kijacho cha wachezaji wa Tanzania.
    “Tumekuwa na furaha tele hivi karibuni kushuhudia mafanikio ya timu ya Taifa ya Vijana ya Tanzania U-17 (Serengeti Boys) na tunawatakia mafanikio mazuri katika michuano inayokuja ya Mataifa ya Afrika (AFCON U-17) nchini Gabon…Kwa programu hii tunaamini tutakuwa tumecheza sehemu muhimu katika harakati pana za kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kutoa timu katika michuano hapa Afrika na Kimataifa kwa miaka mingi ijayo,” alimalizia Legg.
    Hii ni michuano ya pili kwa Azam FC kuandaa kwa upande wa vijana, ambapo mwaka jana iliandaa ile ya chini ya miaka 20 kwa nchi za Afrika Mashariki na kushirikisha timu nne, mbili kutoka Tanzania (Azam FC na Future Stars Academy – Arusha) na Ligi Ndogo Academy (Kenya) na Football For Good Academy (Uganda), huku Azam FC ikiibuka mabingwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC KUANDAA MASHINDANO YA VIJANA KUANZIA U-11 HADI U-17 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top