• HABARI MPYA

    Friday, March 10, 2017

    MLANDIZI QUEENS MABINGWA LIGI YA WANAWAKE

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Mlandizi Queens imefanikiwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Taifa ya Wanawake baada ya ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Panama ya Iringa katika mchezo wa mwisho wa hatua ya Sita Bora ya michuano hiyo iliyodhaminiwa na Azam TV.
    Kwa ushindi huo, Mlandizi Queens ‘Watoto wa Mama Salma Kikwete’ wamemaliza na pointi 15, baada ya kucheza mechi tano na kuwapiku mahasimu wao, JKT Queens waliomaliza nafasi ya pili na Kigoma Stars nafasi ya tatu.
    Shujaa wa Mlandizi Queens leo alikuwa ni kiungo mshambuliaji wao hatari, Mwanahamisi Omar ‘Gaucho’ aliyefunga mabao manne peke yake katika dakika za kwanza, 35, 65 na 76 wakati bao lingine limefungwa na Fadhila Yussuf dakika ya 11.
    Kiungo mshambuliaji wa Mlandizi Queens, Mwanahamisi Omar 'Gaucho' akimtoka beki wa Panama ya Iringa, Asha Malanda  

    Jamila Hassan Kassim akimtoma beki wa Panama 

    Beki wa Panama, Protosia Ngunda akipiga mpira dhidi ya mshambuliaji wa Mlandizi Queens, Rose Mpoma

    Zainab Mlenda wa Mlandizi Queens akiondoka na mpira dhidi ya wachezaji wa Panama

    Kikosi cha Mlandizi Queends kilichoanza leo
    Timu nyingine zilizofuzu hatua ya Sita Bora ni Marsh Queens ya Mwanza iliyomaliza na pointi saba, Fair Play ya Tanga pointi tatu wakati Panama imemaliza bila pointi baada ya kufungwa mechi zote.
    Mlandizi Queens walistahili ushindi huu wa leo kutokana na kucheza vizuri mwanzo hadi mwisho na kwa ujumla, timu hiyo iling’ara tangu mwanzo wa Ligi Kuu ya ya Wanawake hatua ya makundi, inayofanyika kwa mara ya kwanza mwaka huu.
    Michuano hiyo ilianzia hatua ya makundi, Kundi A likiundwa na JKT, Mlandizi, Mburahati, Evergreen, Mtwara na Fair Play wakati Kundi B lilikuwa na Panama, Kigoma, Marsh, Bukoba Queens, Singida Queens na Dodoma Queens.
    Kikosi cha Mlandizi Queens kilikuwa; Janeth Simba, Zainab Mlenda, Shamira Makunguru, Hadija Mohammed, Wema Maile, Asfat Kasindo, Samira Hassan, Grace Mbelayi/Fatuma Issa dk47, Arafa Ramadhan/Rehema Buteme dk60, Mwanahamisi Omar ‘Gaucho’ na Fadhila Yussuf/Rose Mpoma dk72.

    Panama Queens; Edina Ndelwa, Mariam Mbojela, Kapangala Kingamkono, Lucy London, Suzan Komba/Aidan Fukunyula dk84, Asha Malamwa, Eunice Tweve, Maimuna Mtoro/Margareth Luwokozo dk56, Antoneza Mbanga, Neema Nduye na Protosia Mbunda.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MLANDIZI QUEENS MABINGWA LIGI YA WANAWAKE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top