• HABARI MPYA

    Sunday, March 19, 2017

    MAZEMBE YAFA KAMA YANGA, ZESCO YAENDELEA KUNG'ARA

    TP Mazembe imeangukia kwenye kapu la kuwania kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kulazimishwa sare ya 0-0 na wenyeji, CAPS United Uwanja wa Taifa mjini Harare, Zimbabwe.
    Kwa matokeo hayo, Mazembe inatolewa hatua ya 32 Bora ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa bao la ugenini, baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 kwenye mchezo wa kwanza wiki iliyopita mjini Lubumbashi.
    Na sasa inaungana na Yanga SC iliyotolewa na Zanaco ya Zambia na wote watamenyana na timu zilizovuka 32 Bora ya Kombe la Shirikisho kuwania tiketi ya hatua ya makundi.  
    Jesse Were (juu) ameendelea kuifungia mabao Zesco United michuano ya Afrika

    Yanga pia imetolewa kwa bao la ugenini kama Mazembe, baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 Dar es Salaam na kwenda kulazimishwa sare ya 0-0 Lusaka.
    Timu nyingine ya Zambia, Zesco United imeendelea kufanya vizuri hata baada ya kocha wake wa msimu uliopita, George Lwandamina kuchukuliwa na Yanga.
    Zesco jana ilifuzu hatua ya makundi ya Ligi Mabingwa Afrika inayoshirikisha timu 16, baada ya kulazimisha sare ya 2-2 ugenini na Le Messager Ngozi nchini Burundi. 
    Mabao yote manne yalipatikana kipindi cha pili jana Uwanja wa Prince Louis mjini Bujumbura na kufanya mabingwa wa Zambia wasonge mbele kwa ushindi wa jumla wa 4-2 baada ya kushinda 2-0 kwenye mchezo wa kwanza Ijumaa iliyopita mjini Ndola. 
    Oliver Sabumukama alianza kuifungia Le Messager Ngozi dakika ya 49, kabla ya mshambuliaji Mkenya Jesse Were kuisawazishia Zesco dakiak ya 61. 
    Wenyeji wakapata bao la pili kupitia kwa Abdoul Amini dakika ya 86, kabla ya Zesco kusawazisha tena kupitia kwa beki Mkenya, David Owino.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAZEMBE YAFA KAMA YANGA, ZESCO YAENDELEA KUNG'ARA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top