• HABARI MPYA

    Sunday, March 12, 2017

    LWANDAMINA AWAONDOA HOFU WANA YANGA KUHUSU ZANACO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mzambia wa Yanga, George Lwandamina amesema kwamba watafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza jana wakati wakilazimishwa sare ya 1-1 na Zanaco katika mchezo wa kwanza hatua ya 32 Bora Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Yanga ililazimishwa sare ya 1-1 na mabingwa wa Zambia, Zanaco Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na sasa wana wajibu wa kwenda kushinda ugenini ili kuingia hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa.
    Na akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online jana, Lwandamina alisema kwamba mambo machache yalijitokeza jana na kuwaponza kulazimishwa sare ya nyumbani.
    George Lwandamina amesema watafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza jana Yanga ikilazimishwa sare ya 1-1 na Zanaco 

    “Tulitengeneza nafasi nyingi, lakini tukashindwa kuzitumia. Tukafanya makosa yaliyowapa Zanaco nafasi ya kusawazisha bao,”alisema.
    Pamoja na hayo, Lwandamina alisema anaamini Yanga ina nafasi ya kuifunga Zanaco kwao Zambia na kusonga mbele.
    “Mpira haujamalizika, tunajipanga vizuri kwa ajili ya mchezo wao wa marudiano. Sasa tutakaa na kufanyia kazi mapungufu na ubora wa wapizani wetu,”alisema.
    Kwa upande wake, kocha wa Zanaco, Numba Munamba aliwasifu vijana wake kwamba walicheza vizuri. “Kwa sasa tunarudi nyumbani kujipanga na kuhakikisha tunafanyia marekebisho mambo fulani. Nina imani Yanga wakija Zambia tutawafunga,”alisema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LWANDAMINA AWAONDOA HOFU WANA YANGA KUHUSU ZANACO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top