• HABARI MPYA

    Sunday, March 12, 2017

    AZAM FC YAANZA VYEMA AFRIKA, ASANTE SINGANO ‘MESSI’

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    AZAM FC imepata ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Mbabane Swallows katika mchezo wa kwanza wa hatua ya 32 Bora Kombe la Shirikisho Afrika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam usiku huu.
    Shukrani kwake mfungaji wa bao hilo pekee, winga Ramadhani Yahya Singano ‘Messi’ aliyefunga bao hilo dakika ya 84 kwa shuti kali ndani ya 18 baada ya kupokea pasi ya Shaaban Iddi Chilunda.
    Bao hilo lilikuja wakati mashabiki wa Azam FC wakiwa wamekwishakata tamaa na wengine kuanza kuondoka uwanjani, kutokana na mchezo wa kujihami wa wageni.
    Ramadhani Singano 'Messi' akikimbia kushangilia baada ya kufunga bao pekee

    Ramadhani Singano 'Messi' akimtoka beki wa Mbabane Swallows, Sifio Mabila 

    Mshambuliaji wa Azam, Yahya Mohammed akipambana na mabeki wa Mbabane Swallows

    Salum Abubakar 'Sure Boy' akimiliki mpira mbele ya kiungo wa Mbabane, Kabamba Tshishimbi

    Beki wa Azam, Shomary Kapombe akimtoka beki wa Mbabane, Banele Sikhonde
    Mababane Swallows walioingia Uwanja wa Azam Complex kwa ajili ya kutafuta sare tu ya ugenini, wakijilinda zaidi, kupoteza muda na kufanya mashambulizi ya kushitukiza. 
    Na dakika ya 79 almanusra Nahodha wa Swallows, Thulani Tsabedze aifungie timu yake baada ya kumlamba chenga beki Daniel Amoah na kujaribu kumtungua kipa Aishi Manula aliyekuwa ametokea kidogo kwa mbele kwa shuti kali, lakini mpira ukatoka nje.
    Kwa ujumla kilichowanyima mabao mengi Azam FC leo noi kukosa maarifa ya kuupenya ukuta wa Swallows na zaidi sifa zimuendee kiungo Kabamba Tshishimbi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) aliyeiongoza vizuri timu yake katika safu ya kiungo.
    Azam FC sasa itahitaji kwenda kuulinda ushindi wake mwembamba katika mchezo wa ugenini wiki ijayo, kwa kuhakikisha japo inapata sare ili kusonga mbele kuwania kuingia hatua ya makundi.
    Kikosi cha Azam FC kilikuwa: Aishi Manula, Himid Mao, Shomary Kapombe, Bruce Kangwa, Aggrey Morris/Daniel Amoah dk59, Yakubu Mohammed, Joseph Mahundi/Shaaban Iddi dk55, Frank Domayo, Yahaya Mohamed/Khamis Mcha ‘Vialli’ dk75, Salum Abubakar ‘Sure Boy’ na Ramadhani Singano ‘Messi’. 
    Mbabane Swallows: Sandile Ginindla, Thulani Tsabedza, Sifio Mabila, Sanele Mkhweli, Siphamandla Mathenjwa, Mandla Palma, Kabamba Tshishimbi, Wonder Nhleko/Sandile Hlatswako dk86, Sabelo Ndliinisa, Banele Sikhonde na Njabulo Ndlovu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAANZA VYEMA AFRIKA, ASANTE SINGANO ‘MESSI’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top