• HABARI MPYA

    Thursday, March 16, 2017

    ALI KIBA, DIAMOND WAREKODI PAMOJA WIMBO WA SERENGETI BOYS

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    WASANII maarufu wa muziki wa Bongo Fleva, Nassib Abdul ‘Diamond’ na Ali ‘King’ Kiba watarekodi pamoja wimbo maalum wa kuhamasisha kampeni za kuchangia timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys.
    Hayo yamesemwa leo na Mjumbe wa Kamati ya Serengeti Boys, Maulid Kitenge wakati wa mkutano na Waandishi wa Habari leo mchana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuzungumzia mikakati yao ya kukusanya fedha kwa ajili ya kuisaidia timu hiyo.
    Kitenge amesema kwamba tayari ala za wimbo huo zimekwishatengenezwa na wasanii hao wote wametumiwa kwa ajili ya kuingiza sauti, ili mara moja wimbo huo ukamilishwe na kuanza rasmi kusaidia kampeni ya kuhamasisha Serengeti Boys.
    Mjumbe wa Kamati ya Serengeti Boys, Maulid Kitenge akizungumza leo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam 

    “Ali Kiba yuko Marekani na tayari amekwishatumiwa ala za wimbo ili aingize sauti. Na Diamond yeye yupo hapa nchini na tayari ametumiwa ala hizo ili aingize sauti. Wote wameahidi kufanya hivyo mara moja na kurejesha kazi hizo, ili na wasanii wengine waingize sauti zao,”amesema.
    Kitenge amewataja baadhi ya wasanii wengine ambao wataingiza sauti zao kwenye wimbo huo kuwa ni Mwasiti Almasi, Darasa na Vanesa Mdee.   
    Kiba na Diamond wote wapo kwenye Kamati iliyoundwa na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Nape Nnauye ya kuhamasisha na kuwaunganisha Watanzania kwa pamoja ili kuichangia Serengeti Boys iliyofuzu Fainali za Afrika nchini Gabon Mei mwaka huu.
    Katibu wa Kamati hiyo ni Mwesigwa Selestine ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wakati wajumbe ni Kitenge wa EFM Radio na TV, Mkurugenzi wa Mahusiano wa kampuni ya Airtel Tanzania, Beatrice Singano na Mrembo wa Tanzania wa mwaka 1999, Hoyce Temu.
    Pia wamo Mkurugenzi wa Habari katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hassan Abbas; Mkurugenzi wa Global Publishers Limited, Eric Shigongo na Mkurugenzi wa Radio Clouds, Ruge Mutahaba.
    Pamoja na hayo, katika kongamano hilo na wadau wa soka wadau ikiwamo Serikali iliridhia kuwa mshiriki wa karibu kwa kila hatua kuanzia Bodi ya Mfuko wa Maendeleo ya timu za taifa, Kamati ya Hamasa kwa lengo la kupanga pamoja na kushirikiana kwa pamoja.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ALI KIBA, DIAMOND WAREKODI PAMOJA WIMBO WA SERENGETI BOYS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top