• HABARI MPYA

    Saturday, February 11, 2017

    SIMBA KURUDI KILELENI LIGI KUU LEO?

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC itajaribu kurejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara wakati itakapomenyana na Prisons ya Mbeya Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam leo.
    Timu hiyo ya kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog itaingia kwenye mchezo wa leo ikihitaji ushindi tu ili kurejea kileleni mwa Ligi Kuu.
    Na hiyo ni kwa sababu wapinzani wao katika mbio za ubingwa, Yanga SC hawatakuwa na mechi ya Ligi Kuu wikiendi hii kwa kuwa wamekwenda Comoro kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
    Na wakitoka kushinda 3-0 ugenini katika mechi iliyopita ya Ligi Kuu dhidi ya wenyeji Maji Maji mjini Songea, Simba wanajamini kabisa leo wataendeleza wimbi la ushindi.
    Na bila shaka, kocha Omog anayesaidiwa na Mganda, Jackson Mayanja leo ataendelea kupanga safu kali ya ushambuliaji ya wakali watatu, Juma Luizio, Ibrahim Hajib na Mrundi Laudit Mavugo.  
    Kwa ujumla Omog hatarijiwi kufanya mabadiliko makubwa kutoka kikosi kilichoifunga 3-0 Maji Maji Jumamosi Uwanja wa Maji Maji, Songea.
    Na bila shaka langoni ataendelea kusimama Mghana Daniel Agyei, akisaidiwa na beki Mkongo Janvier Bokungu kulia, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ kushoto na katikati Mzimbabwe Method Mwanjali na Novatus Lufunga.
    Viungo wanaweza kuendelea kucheza Muzamil Yassin, Said Ndemla na Shizza Kichuya. Simba SC inashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa pointi zake 48 baada ya kucheza mechi 21, ikiwa nyuma ya mabingwa watetezi, Yanga wenye poinyi 49 za mechi 21.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA KURUDI KILELENI LIGI KUU LEO? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top