• HABARI MPYA

    Sunday, February 12, 2017

    MWANJALI HATARINI KUWAKOSA YANGA FEBRUARI 25

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    BEKI wa kati tegemeo wa Simba, Mzimbabwe Method Mwanjali yuko hatarini kuukosa mchezo dhidi ya mahasimu wa jadi, Yanga Februari 25, mwaka huu.
    Miamba hiyo ya soka nchini, Simba na Yanga itakwaana katika mechi ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Jumamosi ya Februari 25 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Na Mwanjali anaweza kuukosa mchezo huo baada ya kuumia jana katika mechi nyingine ya Ligi Kuu dhidi ya Prisons ya Mbeya, Simba wakishinda 3-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Method Mwanjali akionyesha kuugulia maumivu makali wakati anapatiwa huduma ya kwanza kwenye benchi la Simba

    Mwanjali aliye katika msimu wake wa kwanza Simba SC, alitolewa kwa machela jana na nafasi yake kuchukuliwa na kiungo Mwinyi Kazimoto dakika ya 62.
    Na akiwa kwenye benchi wakati anapatiwa huduma ya kwanza kwenye benchi lao, Mwanjali alionyesha kuugulia maumivu makali.
    Lakini Meneja wa Simba SC, Mussa Hassan Mgosi akasema kwamba kuna muda mrefu kabla ya mechi na Yanga na hatarajii maumivu ya Mwanjali yatakuwa makali kiasi cha kumuweka nje Februari 25.
    “Naona muda bado upo sana, tena wa kutosha. Sitarajii kama atakuwa ameumia kwa kiasi kikubwa,”alisema.
    Mwanjali akitolewa nje kwa machela jana baada ya kuumia katika mchezo dhidi ya Prisons

    Ushindi wa jana uliifanya Simba SC irejee kileleni kwa Ligi Kuu baada ya kufikisha pointi 51 kutoka kwenye mechi 22 na kuwaangushia nafasi ya pili, mabingwa watetezi, Yanga ambao sasa wanabaki na pointi zao 49 za mechi 21.
    Yanga hawakuwa na mechi ya Ligi Kuu wikiendi hii, kwa sababu walikuwa Moroni, Comoro ambao leo wamewafunga wenyeji, Ngaya Club de Mde 5-1 katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Awali Ligi ya Mabingwa Afrika.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWANJALI HATARINI KUWAKOSA YANGA FEBRUARI 25 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top