• HABARI MPYA

    Wednesday, February 08, 2017

    MANJI: KAMA SIFAI, NIMEICHAFUA YANGA, NAWEZA KUONDOKA HATA KESHO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MWENYEKITI wa Yanga, Yussuf Manji amesema kwamba wanachama wa klabu hiyo wanaweza kumuambia aondoke kama wanaona hafai, kufuatia kuhusishwa na tuhuma za kuuza dawa za kulevya. 
    “Na Wanayanga kama mnaona mimi sifai na kama hamna imani na mimi hata kesho naondoka Yanga. Siwezi kuchafua klabu kubwa,”.
    Pamoja na hayo, Manji amesema anaogopa kwenda Comoro na Yanga, kwa sababu ataambiwa amepeleka dawa za kulevya.
    Yanga wanatarajiwa kuwa wageni wa Ngaya Club Jumapili nchini Comoro katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Awali Ligi ya Mabingwa Afrika na walipanga kuondoka Ijumaa. 
    Na akizungumza katika mkutano na waandishi wa Habari mjini Dar es Salaam jana jioni, muda mfupi baada ya kutajwa kwenye orodha ya watu 65 wanaoshukiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya, Manji alisema; “Hii itanifanya nishindwe kwenda Comoro na Klabu ya Yanga sababu wa Comoro watasema nimepeleka madawa. Wananichafua sana,”alisema.
    Mapema jana, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alitaja orodha ya watu wanaoshukiwa kujihusisha na dawa za kulevya, Manji ambaye pia ni Diwani wa Mbagala Kuu akiwa miongoni mwao pamoja na Mbunge wa zamani wa Kinondoni, Idd Azzan, aliyewahi pia kuwa Katibu wa Simba.  
    Na kwa pamoja washukiwa wote 65 wametakiwa kufika makao makuu ya Jeshi la Polisi Saa 5:00 asubuhi siku ya Ijumaa kwa mahojiano juu ya shutuma hizo. Lakini Manji alisema; “Mimi nitakwenda kituo cha Polisi kesho, sisubiri hiyo Ijumaa,”.
    Akaongeza; “Chaguzi zilizopita mimi nilichukuahukua fomu peke yangu ya kugombea Yanga hivyo naheshimika. Huwezi kunitangaza kupitia Redio kwamba niende kwenye kituo cha Polisi saa tano. Makonda ni mdogo kwangu kiumri,”alisema Manji.
    Manji alisema Katiba inasema kila mtu ana haki yake, hivyo akichafuliwa yeye kama Mwenyekiti wa Yanga na klabu hiyo inachafuliwa pia.
    “Kifungu cha 66 katika katiba kinaeleza haki zangu na kifungu cha 32 pia. Vinanilinda. Ninataka nimshitaki Mahakamani na vyombo vyote vilivyoandika kunituhumu na madawa. Kesho naenda Polisi asubuhi nihojiwe baada ya hapo ninaanza kutafuta haki yangu. Huwezi kuniita kaka huku unanitaja kwenye mambo mabaya,”alisema.
    Manji amemshangaa Makonda kwa nini hajawaita viongozi wa dini kama Askofu Polycarp Pengo au Mashehe wamsaidie katika hilo.
    “Huwezi kuniita mimi kama mbwa...njoo, hii ni kutafuta masifa. Kesho utanikuta mimi kwenye gazeti na wengine 65 watasahaulika. Hii sio haki. Zipo njia za kushughulikia vitu, Tukienda Comoro tunaenda na bendera ya Tanzania,”.
    Manji alisema kwamba yupo tayari kupimwa na kusachiwa na Makonda naye apimwe kama anatumia na wamsachi pia.
    “Mimi sitaki kuchanganya vitu viwili kwenye mkutano mmoja. Kesho au keshokutwa ntafanya mkutano kuanzia PSPF, Coco Beach na kadhalika. Leo nakaa kwenye point moja tu ya madawa.
    “Mkuu wa mkoa kunasehemu nimegongana naye oysterbay na nlienda kuonanana naye kama diwani wa mbagala kuu kumuomba mkuu wa majeshi atakayekuja ahamishe kambi ya jeshi kutoka mbagala na kupelekwa nje ya mji. Kama diwani siwezi kumuandikia rais,”.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MANJI: KAMA SIFAI, NIMEICHAFUA YANGA, NAWEZA KUONDOKA HATA KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top