• HABARI MPYA

    Tuesday, February 07, 2017

    LWANDAMINA: WACOMORO WATATUPA SUMU YA KUIMALIZA SIMBA

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KOCHA wa Yanga, Mzambia George Lwandamina amesema kwamba mechi mbili dhidi ya Ngaya Club ya Comoro zitawapa picha nzuri ya timu yao kabla ya kuvaana na Simba Februari 25, mwaka huu.
    Yanga watamenyana na mahasimu wa jadi, Simba SC Februari 25, mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Na akizungumza na Bin Zubeiry Sports - Online juzi, Lwandamina alisema kwamba mapema mno kuizungumzia mechi na Simba, kwa sababu kwanza wana mechi za Ligi ya Mabingwa.
    “Kwanza tuna mechi na Wacomoro, tutacheza nyumbani na ugenini, mechi ambazo zitatupa picha nzuri kabla ya kucheza na Simba,”alisema.
    Yanga watakuwa wageni wa Ngaya FC Jumapili mjini Ngaya kabla ya kurudiana wiki inayofuata Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na baada ya hapo watakwenda mafichoni kwa ajili ya mchezo dhidi ya Simba, Februari 25. 
    Mbio za ubingwa wa Ligi Kuu zimeshika kasi kwa sasa, miamba miwili ya soka nchini Simba na Yanga ikifukuzana kileleni.
    Kwa sasa, Yanga SC wapo kileleni mwa Ligi Kuu kwa pointi zao 49, wakifuatiwa na Simba SC yenye pointi 48 lakini baada ya timu zote kucheza mechi 21.
    Na hiyo ni baada ya matokeo mazuri kwa timun zote mwishoni mwa wiki, Yanga wakianza kuiadhibu Stand United kwa mabao 4-0 Uwanja wa Taifa, Ijumaa na Simba wakafuatia kwa kuitandika Maji Maji 3-0 Uwanja wa Maji Maji Songea Jumamosi.
    Wakati mabao ya Yanga Ijumaa yalifungwa na Donald Ngoma, Simon Msuva, Obrey Chirwa na Nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’, ya Simba SC Jumamosi yalifungwa na Ibrahim Hajib, Said Ndemla na Laudit Mavugo.
    Mara ya mwisho timu hizo zilikutana katika Nusu Fainali ya Kombe la Mapinduzi Januari 10, mwaka huu Uwanja wa Amaan, Zanzibar na Simba ikashinda kwa penalty 4-2 baada ya sare ya 0-0 ndani ya dakika 90.
    Awali ya hapo, katika mchezo wa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Oktoba 1, mwaka huu na kutoka sare ya 1-1, Yanga wakitangulia kwa bao la Amissi Tambwe kipindi cha kwanza kabla ya Simba kusawazisha kwa bao la Shizza Kichuya kipindi cha pili.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LWANDAMINA: WACOMORO WATATUPA SUMU YA KUIMALIZA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top