• HABARI MPYA

    Saturday, January 07, 2017

    OMOG AWAPIGIA HESABU KALI JANG'OMBE BOYS

    Na Mwandishi Wetu, ZANZIBAR
    KOCHA wa Simba, Mcameroon Joseph Marius Omog amesema kwamba anatarajia upinzani mkali kesho kutoka kwa Jang’ombe Boys katika mchezo wa mwisho wa Kundi A Kombe la Mapinduzi.
    Akizungumza mjini hapa jana, Omog alisema kwamba Jang’ombe Boys ni timu nzuri na ilidhihirisha hilo baada ya kuwafunga mabingwa watetezi, URA 2-1, hivyo hata mbele ya Simba watakuwa tishio tu.
    Kwa sababu hiyo, Omog amesema kwamba amewandaa vizuri vijana wake kwenda kucheza kwa tahadhari ili kuepuka kuingia kwenye mitego ya Jang’ombe Boys.
    Kocha Joseph Omog akiwa na Msaidizi wake, Mganda Jackson Mayanja (kulia) 

    “Utakuwa mchezo mgumu. Hiyo timu (Jang’ombe Boys) imewafunga wanaoshikilia Kombe, imefunga timu nzuri ambayo sisi tumetoka nayo sare, kwa huyo tunauelekea mchezo mgumu na tutacheza kwa tahadhari tupate matokeo mazuri twende Nusu Fainali,”alisema Omog.
    Simba SC inaongoza Kundi A kwa pointi zake saba, baada ya kushinda 2-1 dhidi ya Taifa Jang’ombe, 1-0 dhidi ya KVZ na sare ya 0-0 na URA. Jang’ombe Boys wanafuatia kwa pointi zao sita sawa na Taifa Jang'ombe, wakati URA inashika mkia kwa pointi zake nne.
    Hadi sasa hakuna timu yenye uhakika wa Nusu Fainali katika Kundi hilo, ikiwa URA inaweza kufikisha pointi za saba za Simba na Jang’ombe Boys na Taifa wanaweza kumaliza na pointi tisa.
    Wakati huo huo: Mshambuliaji wa Simba, Frederick Blagnon raia wa Ivory Coast jana alitarajiwa kujiunga na wenzake kambini baada ya kupona. Mchezaji huyo alichelewa kujiunga na wenzake kwenye kambi ya Kombe la Mapinduzi kutokana na kuwa mgonjwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OMOG AWAPIGIA HESABU KALI JANG'OMBE BOYS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top