• HABARI MPYA

    Friday, January 13, 2017

    ASHANTI NA FRIENDS RANGERS JUMAPILI KARUME KOMBE LA ASFC

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MICHUANO ya kuwania Kombe la Shirikisho ya Azam (Azam Sports Federation Cup 2016/2017), inatarajiwa kuendelea kesho kwa kukutanisha timu za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) baada ya hatua ya kushirikisha timu za daraja la pili na timu za ligi ya mikoa (RCL) kukamilika.
    Kesho Jumamosi Januari 14, mwaka huu, KMC ya Kinondoni itacheza na Kiluvya United ya Pwani kwenye Uwanja wa Karume, Dar es Salaam kabla ya keshokutwa Jumapili Januari 15, mwaka huu kwenye viwanja tofauti.
    Mechi nyingine za Jumapili ni kati ya Ashanti United na Friends Rangers – zote za Dar es Salaam mchezo utakaofanyika Uwanja wa Karume ulioko Ilala jijini wakati Coastal Union itacheza na Mgambo JKT kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga.
    Panoni ya Kilimanjaro itaikaribisha African Sports ya Tanga kwenye Uwanja wa Ushirika Moshi wakati Alliance itacheza na Pamba kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza huku Mbeya Warriors ikiikaribisha Kimondo kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.
    Kurugenzi itacheza na Kiluvya kwenye Uwanja wa Mafinga wakati kwenye Uwanja wa Karume Musoma, Rhino ya Tabora itakuwa mgani wa Polisi Mara ilhali Singida United itakuwa mwenyeji wa Mvuvumwa ya Kigoma kwenye Uwanja wa Namfuta.
    Polisi ya Morogoro itacheza na timu  nyingine ya Polisi kutoka Dodoma kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro wakati kwenye Uwanja wa Njombe, Njombe Mji itacheza na JKT Mlale kutoka Songea wakati Polisi Dar itacheza na Mshikamano Jumatatu ya Januari 16, mwaka huu.
    Kwa mechi zilizocheza jana Januari 12, 2017 Madini ya Arusha ambayo iliilaza Mirambo ya Tabora mabao 4-0 sasa itaivaa Oljoro iliyoshinda kwa penalti 4-3 dhidi ya Mawenzi baada ya kumaliza dakika 90 kwa sare ya bila kufungana. Mechi hiyo itafanyika kesho kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha.
    Timu zilizotangulia na kusubiri washindi wa michezo ya leo ni Kabela City ya Shinyanga ambayo iliifunga Murusagamba ya Kagera mabao 4-0 katika mchezo uliofanyika Kahama huko mkoani Shinyanga.
    Kwa hiyo, Kabela City sasa inasubiri mshindi kati ya Jangwani ya Rukwa na Stand Bagamoyo ya Pwani ambazo zinacheza leo Januari 13, mwaka huu katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Mandela ulioko Msata mkoani Pwani.
    Timu nyingine iliyotangulia ni Changanyikeni ya Dar es Salaam iliyoifunga Burkina Faso ya Morogoro bao 1-0 katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam. Changanyikeni sasa inasubiri mshindi kati ya Green Warriors ya Pwani na Cosmopolitan ya Dar es Salaam ambazo leo zinacheza Uwanja wa Karume.
    Baada ya Namungo FC ya Lindi kutojitokeza Uwanja wa Majimaji, timu ya The Mighty Elephant ya Songea ilipewa ushindi na kwa sasa inasubiri mshindi kati ya Mashujaa ya Kigoma ambayo leo inacheza na Kitayosa ya Kilimanjaro kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika.    
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ASHANTI NA FRIENDS RANGERS JUMAPILI KARUME KOMBE LA ASFC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top