• HABARI MPYA

    Thursday, December 15, 2016

    SIMBA WAIFUATA NDANDA KIKAMILIFU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIKOSI cha Simba kimeondoka leo asubuhi Dar es Sakaam kwenda Mtwara tayari kwa mchezo wake wa kwanza wa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara. 
    Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya klabu hiyo, Hajji Sunday Manara ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba timu imeondoka na wachezaji 
    20 kwa ajili ya mchezo huo.
    Simba watakuwa wageni wa Ndanda FC Jumapili Uwanja wa Nangwanda, Sijaona, Mtwara katika fungua dimba ya duru la pili la Ligi Kuu.
    Na ingawa Manara hakutaja wachezaji walioongozana na timu mjini humo, lakini Bin Zubeiry Sports – Online inafahamu ambao hawajakwenda kwa sababu mbalimbali ni Juuko Murshid, Mwinyi Kazimoto, Mussa Ndusha, Pastory Athanas, Emmanuel Semwanza na kipa Vincent Angban.
    Muivory Coast Angban na Ndusha kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wanaachwa baada ya kusajiliwa wachezaji wapya kutoka Ghana, kipa Daniel Agyei na kiungo James Kotei. 
    Murshid bado yuko na timu yake ya taifa ya Uganda, Mwinyi Kazimoto ni majeruhi, Pastory Athanas hajakamilisha uhamisho wake kutoka Stand United na Emmanuel Semwanza ana matatizo ya kifamili.
    Wachezaji wanaotarajiwa kuwamo kwenye msafara ni makipa; Daniel Agyei, Peter Manyika, mabeki; Hamad Juma, Janvier Bokungu, Abdi Banda, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Novaty Lufunga na Method Mwanjali.
    Viungo ni James Kotei, Jonas Mkude, Said Ndemla, Muzamil Yassin, Jamal Mnyate, Shizza Kichuya na washambuliaji Frederick Blagnon, Laudit Mavugo, Ibrahim Hajib, Juma Luizio na Hajji Ugando.
    Simba ilimaliza mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara katika nafasi ya kwanza kwa pointi zake 35, mbili zaidi ya mabingwa watetezi, Yanga. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA WAIFUATA NDANDA KIKAMILIFU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top