• HABARI MPYA

    Sunday, December 18, 2016

    SAMATTA AFUNGA LA KUSAWAZISHA NA KUINUSURU GENK KULALA KWA STANDARD LIEGE

    Na Mwandishi Wetu, GENK
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta leo ameinusuru timu yake, KRC Genk kulala nyumbani mbele ya Standard Liege katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji.
    Samatta ameifungia bao la kusawazisha Genk katika sare ya 2-2 na Liege Uwanja wa Laminus Arena mjini Genk.
    Na mchezaji huyo wa zamani wa Simba alifunga bao hilo dakika ya 77 akimalizia pasi ya beki Jere Uronen kutoka Finland.
    Katika mchezo huo, ambao mshambuliaji wa Uganda, Faruk Miya alikuwa kwenye benchi la Liege muda wote, Genk walikuwa wa kwanza kupata bao lililofungwa na beki Mgambia Omar Colley dakika ya tatu, akimalizia pasi ya mshambuliaji Mjamaica, Leon Bailey.
    Samatta (kushoto) akikimbia kushangilia baada ya kuifungia bao la kusawazisha Genk katika sare ya 2-2 na Liege Uwanja wa Laminus Arena mjini Genk

    Standard Liege ikatoka nyuma na kuongoza kwa 2-1 kwa mabao ya washambuliaji Mreno Orlando Sa dakika ya 15 na Mualgeria Ishak Belfodil dakika ya 25.
    Huo unakuwa mchezo wa 35 jumla kwa Samatta kucheza Genk tangu awasili Januari mwaka huu kutoka TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC),18 msimu uliopita na 17 msimu huu. 
    Kati ya hizo, ni mechi 17 tu alianza, 10 msimu uliopita na saba msimu huu, 18 alitokea benchi, nane msimu uliopita na 10 msimu huu, wakati nane hakumaliza baada ya kutolewa, sita msimu uliopita na mbili msimu huu huku akiwa amefunga jumla ya mabao tisa, manne msimu huu na matano msimu uliopita.
    Kikosi cha KRC Genk kilikuwa; Bizot, Walsh/Uronen dk76, Colley, Dewaest, Castagne, Ndidi, Pozuelo, Samatta, Trossard/Buffalo dk72, Bailey na Karelis.
    Standard Liege : Hubert, Goreux, Elderson, Raman/Mbenza dk39, Edmilson/Fiore dk81, Trebel, Kosanovic, Laifis, Cisse, Sa/Dompe dk63 na Belfodil.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA AFUNGA LA KUSAWAZISHA NA KUINUSURU GENK KULALA KWA STANDARD LIEGE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top