• HABARI MPYA

    Friday, November 11, 2016

    WATANO ZANZIBAR WAFAULU MCHUJO WA KUJIUNGA NA U-17 YA AZAM

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    WACHEZAJI watano Zanzibar wamechaguliwa kujiunga na timu ya vijana chini ya umri miaka 17 ya Azam FC baafa ya usajili uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita visiwani humo.
    Vijana hao wameingia kwenye mchujo wa mwisho utakaofanyika mwezi ujao makao makuu ya Azam, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam yakihusisha vijana wote waliochaguliwa kwenye mikoa mbalimbali.
    Vijana hao watano wanaungana na wengine 37 waliochaguliwa kwenye maeneo tofauti nchini katika mikoa ya Morogoro (12), Dar es Salaam (13), Tanga (12) na kufikisha idadi ya vijana 42 waliochaguliwa mpaka sasa kati ya vipaji 2,143 waliofanyiwa usaili.
    Uongozi wa Azam FC kwa kushirikiana na idara ya ufundi ya timu hiyo, umedhamiria kuboresha mfumo wa kituo chake cha kukuza vipaji 'Azam FC Academy' ili kihusishe vijana wa umri tofauti kwa ajili ya kuvuna vipaji vingi zaidi kwa manufaa ya baadaye ya timu hiyo na Taifa kwa ujumla.
    Hadi sasa Azam FC imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kwenye uleaji wa vipaji katika kituo hicho, ikivuna vijana kadhaa wanaotamba sehemu tofauti katika timu mbalimbali nchini, wengine wakiwa wanaing'arisha timu kubwa ya kituo hicho.
    Baadhi ya waliopandishwa kwenye timu kubwa ni makipa Aishi Manula, Metacha Mnata, mabeki Ismail Gambo, Gadiel Michael, Abdallah Kheri (mkopo Ndanda), viungo Mudathir Yahya, Masoud Abdallah, Bryson Raphael (mkopo Ndanda).
    Wengine ni Joseph Kimwaga (mkopo Mwadui), Farid Mussa (aliye mbioni kujiunga na CD Tenerife - Hispania), wshambuliaji Kelvin Friday (mkopo Mtibwa Sugar) na Shaaban Idd.
    Wanaotamba na timu nyingine baadhi yao ni Simon Msuva (Yanga), Mohamed Hussein (Simba), Rashid Mandawa (Mtibwa Sugar), Joseph Mahundi (Mbeya City), Jamal Mnyate (Simba).
    Wakati huo huo: Azam FC, inatarajia kuendelea kusaka wachezaji chini ya umri wa miaka 17 Jumamosi ijayo Novemba 12 mwaka huu kuanzia saa 2.00 asubuhi hadi saa 9.00 alasiri ndani ya Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.
    Baada ya wikiendi iliyopita kufanya majaribio ya wazi visiwani Zanzibar, ambako walichaguliwa wachezaji watano, sasa tunarudisha mkazo wetu Tanzania Bara na kufanya majaribio ya mwisho katika jiji la Dar es Salaam.
    Kwa majaribio mengine ya wazi katika maeneo mengine kuzunguka Tanzania yatatangazwa hivi karibuni.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WATANO ZANZIBAR WAFAULU MCHUJO WA KUJIUNGA NA U-17 YA AZAM Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top